Breaking News

TANGA URITHI FESTIVAL YAKA NA UCHUMI WA BULUU

Tanga Urithi Festival yaja na Uchumi wa 'buluu,'  fursa bwerere kwa Wawekezaji. 

 Balozi wa Japani nchini Tanzania akaribishwa Tanga kunywa Chai ya Nazi. 

 Dua ya kumuombea Rais kufanyika Tanga Urithi Festival, pia utakuwepo mdahalo wa Kumbukizi ya Shaban Robert, magwiji lugha ya Kiswahili kukutana.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi Dkt Batilda Salha Burian akizungumza katika mkutano wake na Waandishi wa Habari Disemba 25, 2024 kuhusu tamasha hilo.
Majadiliano kuhusu tamasha hilo yakiendelea.

.....................................

Mashaka Kibaya, Tanga 

BALOZI wa Japani nchini Tanzania na familia yake ni miongoni mwa wageni wanaotarajiwa kunogesha tamasha la Tanga Urithi Festival linalotarajiwa kufanyika katika Halmashauri ya Jiji la Tanga kuanzia Disemba 27 mwaka huu na kutamatishwa Januari Mosi.

Taarifa hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi Dkt Batilda Salha Burian katika Mkutano wake na Waandishi wa Habari akisema, Disemba 28 Balozi wa Japani na wageni wengine watapata fursa ya kuonja Chai mbalimbali zinazotumiwa na Wakazi wa Mkoa wa Tanga.

"Tarehe 28 itakuwa Uchumi wa buluu kwenye ratiba yetu, Balozi wa Japani atakuja na familia yake na kutakuwa 'Tea Party' ambapo Balozi na wageni wengine watapata fursa kuonja Chai mbalimbali tunazotumia kama Chai ya Nazi,nanasi, Chai ya pilipili na alkasusi"alisema RC Tanga.

Tanga Urithi Festival pia itatoa fursa ya kufanyika kwa Dua ya kumuombea Rais Dkt Samia Suluhu Hassan na Watanzania wote huku kukitarajiwa kufanyika kwa mdahalo wa Kumbukizi ya nguli wa lugha ya Kiswahili Marehemu Shaban Robert.

Kupitia Mkutano wake huo na wanahabari,RC Balozi Dkt Batilda Salha Burian amewakaribisha watu wote kushiriki tamasha hilo,akisema Wawekezaji wanaweza kuja Tanga kama eneo mojawapo la kimkakati.

Amesema, kwa kuja Tanga wanaweza kuona fursa kwenye Uchumi wa buluu,uchimbaji wa madini ya Vito na yale ya viwandani,fursa katika uwekezaji nyumba za makazi,hoteli za ngazi mbalimbali,uwekezaji kwenye elimu,maeneo ya biashara na hata yale ya michezo.

Pia tamasha litatoa fursa kwa Vijana na watu kutoka makundi maalum wenye mawazo mazuri ya biashara huku wakishindwa  kuyaendeleza ambapo watawezeshwa hatua ambayo itawasaidia katika kukimarisha kiuchumi.

"Wote wanaopenda utamaduni asilia wanapaswa kushiriki, Wajasiriamali na Wawekezaji wanaotafuta fursa wanapaswa kushiriki,watu wa uvumbuzi na wengine wote" alisema Mkuu huyo wa Mkoa wa Tanga Balozi Dkt Batilda. 

Taarifa ya Mkuu wa Mkoa iliendelea kueleza kuwa,tamasha la Tanga Urithi Festival litahusisha urithi wa chakula,burudani,michezo ambapo pia kutakuwa na Usiku wa Kanga za kale na burudani asilia zitakayochagizwa na taarabu.

"Kutakuwa na Usiku wa alwatani,usiku wa mvuvi huku mavazi mbalimbali yakipamba siku hiyo, mavazi ya Kanga,baibui,msuli na baraghashia kwa Wanaume na mavazi mengine asilia"alisema Mkuu wa Mkoa.

Mkuu huyo wa Mkoa alisema, tayari watu kutoka Zanzibar wamekuja na rasmi na taarabu yenye Vifaa na Zana za kitamaduni huku kukitarajiwa kuwa na Ngoma asilia kama Mdumange na nyingine kutoka Mkoani hapo.

"Pia kutakuwa na michezo kama vile bao na mingine mingi kutoka Mwambao wa Pwani,chakula cha Mwambao,nyama choma,Samaki nk"alisema Mkuu wa Mkoa wa Tanga.

Pamoja na hayo,Balozi Dkt Batilda kutakuwa na siku huru kwa ajili ya watu wote kwenda kutembelea utalii likiwemo eneo la Marine Park ya Samaki aina ya Silikanti.

No comments