Breaking News

WAPIGA KURA 37, 655, 559 KUSHIRIKI UCHAGUZI MKUU 2025

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufani Jacobs Mwambegele akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutanio wa Tume na Wazalishaji Maudhui Mtandaoni kuhusu uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025. Kikao hicho cha siku moja kilifanyika jijini Dar es Salaam leo Agosti 03 , 2025.

.....................................

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

JUMLA ya wapiga kura 37,655,559 wanatarajia kushirikia katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2025, huku wapiga kura 36,650,932 wakitokea Tanzania Bara na wapiga kura 1,004,627 wakitokea Tanzania Zanzibar.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi wa Tume Huru ya Uchaguzi (INEC), Kailima Ramadhani wakati akiwasilisha mada katika mafunzo kwa wanahabari wazalishaji wa maudhui mitandaoni ambayo yamefanyika leo Ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam.

Kailima aliwataka wazalishaji wa maudhui mitandaoni kutoa taarifa kuhusu mchakato wa uchaguzi mkuu wa mwaka huu ili wananchi wajue hatua mbalimbali kuelekea uchaguzi huo.

Alisema kauli mbiu ya uchaguzi wa mwaka huu ni “Kura Yako Haki Yako, Jitokeze Kupiga Kura” na kwamba imelenga kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi siku ya tarehe 29 Oktoba, 2025 kwa ajili ya kupiga kura.

Mwenyekiti wa Tume hiyo Jaji wa Mahakama ya Rufaa Jacobs Mwambegele akifungua mafunzo hayo aliwahimiza wazalishaji wa maudhui mtandaoni kutumia majukwaa yao kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kupiga kura. 

Alisema Tume inatambua mchango mkubwa wa wazalishaji wa maudhui mtandaoni kwanza ikiwa ni daraja la mawasiliano kati ya Tume na wananchi na wadau wengine na  pili wakiwa ni wadau wa moja kwa moja wa mchakato wa uchaguzi huo.

 

Kwa upande wake  Meneja wa Kitengo cha Huduma za Utangazaji kutoka TCRA, Mhandisi Andrew Kisaka, aliwataka  Wazalishaji wa maudhui mtandaoni kuepuka kuchapisha taarifa zinazoweza kusababisha taharuki au kuchochea machafuko.

 Wakati wa uchaguzi huwa kuna kuwa na changamoto nyingi za kiitikadi za kisiasa na hivyo kusababisha mivutano ambayo wakati mwingine inatoa matukio mabaya hivyo waandishi wa habari mnapaswa kuwa wazalendo wakati wa kuchukua taarifa zenu kwani wakati mwingine huwa zinachochea vurugu badala ya kusaidia” alisema

Aidha, Kisaka aliwataka watoa mahudhui hao kujiepusha kusambaza uvumi,  kutopendelea upande wowote na kuweka ushabiki kwa chama chochote na kutumia lugha nzuri.Mkurugenzi wa Tume Huru ya Uchaguzi (INEC), Kailima Ramadhani, akiwasilisha mada kwenye mkutano huo.Meneja wa Kitengo cha Huduma za Utangazaji kutoka TCRAMhandisi Andrew Kisaka, akitoa mada kwenye mkutano huo.


Viongozi meza kuu wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya washiriki wa mkutano huo.
Washiriki wakiwa kwenye mkutano huo.
Mkutano ukiendelea.

 Mkutano ukiendelea.

No comments