Breaking News

UMOJA WA WAISLAM RAIA WA AFRIKA KUSINI WATOA MSAADA WA VITI MWENDO ZANZIBAR


 Watoto wenye uhitaji wakiwa na wazazi wao baada ya kukabidhiwa viti mwendo vilivyotolewa na Umoja wa Waisam raia wa Afrika Kusini katika hafla iliyofanyika jana Septemba 19, 2025 eneo la Migombani Zanzibar.

....................................

Na Dotto Mwaibale, Zanzibar 

UMOJA wa Wafanyakazi Waislam Raia wa Afrika Kusini wanaofanya kazi Dubai kwa kushirikiana na Hussein Ramadhani Layya (Maarufu Msokolo) wametoa msaada wa viti mwendo kwa watoto 50 wenye uhitaji maalumu katika hafla iliyoandaliwa na Baraza la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar.

 Akizungumza katika hafla hiyo, Msokolo alisema msaada huo uliotolewa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi, katika kuboresha maisha ya watu wenye ulemavu.

"Tunapotoa msaada huu kwa wenzetu hawa tunapaswa kukumbuka kuwa sisi sote tuna udhaifu na  changamoto zinazoweza kudhoofisha miili yetu hivyo, tusisahau kuwa hakuna aliye bora kuliko mwingine, maisha yetu yana thamani, bila kujali hali ya mtu, umri, jinsia au ulemavu,” alisema Msokolo.

Alisema msaada huo unakwenda kutoa faraja kwa walengwa ambapo aliomba ushirikiano huo wa pamoja uzidi kuendelea baina ya umoja huo na wananchi kwa ujumla wao.

Aidha, Msokolo alisema kuwa tukio hilo linatuacha na funzo kubwa kwamba utu, mshikamano na upendo ni silaha kuu za kujenga jamii yenye uhitaji na ni heshima kubwa.

Aliongeza kuwa kila kiti mwendo kilichotolewa si msaada pekee, bali ni daraja la matumaini na uthibitisho kwamba kila mtoto ana haki ya kuishi kwa heshima.

"Maisha ya kila mmoja wetu ni zawadi na thamani yake haipimwi kwa udhaifu, bali kwa fursa ya kuonyesha upendo na tunapo wakumbatia wenzetu wenye changamoto, tunamshukuru Mungu kwa zawadi ya utu wetu sote,” alisema Msokolo .

 Aliongeza kwamba msaada huo ni ishara ya mshikamano wa kimataifa na unaunga mkono maono ya Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi, ya kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata heshima, nafasi na huduma wanazostahili.

Kwa upande wake Mwakilishi wa umoja huo, Ahmed Kathrada alisema kwamba utoaji wa msaada huo ni hatua njema ya kuonesha upendo kwa wahitaji ambao ni jamaa na ndugu zetu ambao ttupo nao katika familia zetu.

"Nilipata hamasa nilipoona ndugu yangu Msokolo akikabidhi fimbo kwa ndugu zetu wenye changamoto ya uoni hafifu mwaka jana. Nilipiga simu kwa wenzangu Dubai, na kwa dakika tano tukawa tumepata fedha za kununua viti mwendo 50. Huu ni mwanzo tu – tutaendelea kuwasaidia watu wenye uhitaji maalumu Zanzibar." Alisema Kathrada.

 Katibu wa Baraza la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar, Ussi Khamis Debe, akkizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo aliupongeza umoja huo kwa msaada walioutoa na kueleza umegusa nyoyo za walengwa.

"Mmetuletea faraja kubwa kwa watoto wetu tunawashukuru sana Umoja wa Wafanyakazi Waislam kutoka Dubai pamoja na ndugu yetu Msokolo, " alisema Debe.

.................................................. 

Kuhusu Ulemavu Zanzibar 

Takwimu za Ulemavu Zanzibar (Sensa ya 2022): 

Idadi ya watu wenye ulemavu: 145,497 (11.4% ya wakazi wote) 

Wanaume: 61,375 

Wanawake: 84,222 

Tafiti za UNICEF zinaonyesha miongoni mwa changamoto zinazowakabili watoto na vijana ni: 

Ugumu wa kusikia – 0.8% 

Ugumu wa kuongea/kuwasiliana – 1% 

Ugumu wa kujitunza – 1.6% 

Ugumu wa kutembea – 0.6% 

Ugumu wa kukumbuka – 1%

Hussein Ramadhani Layya (Maarufu Msokolo kushoto) akizungumza wakati wa kutoa msaada huo. Wengine ni viongozi wa umoja wa waislam raia wa Afrika Kusini waliowezesha msaada huo.

Msaada ukitolewa.
Viongozi mbalimbali wa Umoja wa Waislam raia wa Afrika Kusini wakiwa katika picha ya pamoja na watoto wenye uhitaji baada ya kuwakabidhi viti mwendo.
Hussein Ramadhani Layya (Maarufu Msokolo mwenye shati jeusi ) akizungumza na wazazi na walezi wa watoto wenye uhitaji wakati wa kuwakabidhi msaada wa viti mwendo.
Mtoto akiwa na kiti mwendo chake baada ya kukabidhiwa.
 

No comments