Breaking News

POLISI TANZANIA YANG’ARA KIMATAIFA, ASKARI WAKE ATUNUKIWA TUZO YA BALOZI WA AMANI DUNIANI

Mrakibu wa Polisi (SP) Balozi Dkt. Ezekiel Abernego Kyogo kutoka Makao Makuu ya Jeshi la Polisi Tanzania, akionesha Tuzo Balozi wa Amani Duniani (AMB) "Peace Ambassador (AMB)" na Greenling Peace Foundation. baada ya kutunukiwa.

.................................................

Na Dotto Mwaibale, Dar es Salaam

NENO Amani ni neno ambalo limezoeleka sana miongoni mwa jamii na limekuwa likizungumzwa na kila mtu wakiwemo viongozi wa kisiasa na dini kutokana na umuhimu wake.

Mahala popote ambapo hapana Amani hapawezi kufanyika jambo lolote la maendeleo kama tunavyoona nchi nyingi duniani ambazo Amani imetoweka kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo vita za kugombea madaraka na mali.

Kutokana na kutambua umuhimu wa Amani duniani kote kuna baadhi ya watu wamekuwa wakijitolea au kufanya kazi ya kuhimiza kudumisha Amani kwani mara nyingi inapokosekana na kuzuka vita au vurugu wanaokuwa kwenye changamoto kubwa ni watoto na wanawake.

Nchini Tanzania mmoja wa watu ambaye amekuwa akilipigania Taifa letu liwe na Amani ni Ezekiel Kyogo.

Jina la Ezekiel Kyogo siyo jina jipya hapa nchini kutokana na kazi kubwa anayoifanya ya kuhubiri Amani,

Ezekiel Kyogo ni Mrakibu wa Polisi (SP) kutoka Makao Makuu ya Jeshi la Polisi Tanzania ambaye amepewa heshima anayostahili kwa kutunukiwa Tuzo Balozi wa Amani Duniani (AMB) "Peace Ambassador (AMB)" na Greenling Peace Foundation.

Balozi Dkt. Kyogo amethubutu, ameonesha njia na kuliheshimisha Jeshi la Polisi nchini kwa utoaji wa elimu, uhamasishaji utunzaji wa amani na kubeba bendera ya Taifa kimataifa na kwenye majukwaa makubwa duniani. 

SP Kyogo anafanyakazi Kamisheni ya Polisi Jamii Kitengo cha Ushirikishwaji wa jamii na kazi ya kitengo hicho ni kuelimisha jamii mambo mbalimbali ya amani, uzalendo na usalama ili kuifanya Tanzania kuwa salama. 

Tuzo hizo zilitolewa na Mwenyekiti Mwanzilishi wa Greeling Global Peace Organization Zambia Prof Bishop Kennedy Songwe pamoja na mgeni rasmi wa hafla ya utoaji wa tuzo hiyo Balozi Prof. Askofu Rejoice Ndalima.

Katika hafla ya kutunuku tuzo hizo iliyofanyika Ukumbi wa Rungwe Hotel Jijini Dar es Salaam Novemba 29, 2025 , ilihudhuriwa na wageni waalikwa, wawakilishi wa taasisi mbalimbli, wanaharakati wa amani na viongozi wa kimataifa.

Kutunukiwa kwa Tuzo hiyo hakukuwa kwa kubahatisha kunatokana na kazi kubwa anayoifanya kwa makundi mbalimbali ya kutoa elimu ya kuitunza Amani na mchango wake mkubwa uliotukuka katika Taifa juu ya Amani.

Sehemu kubwa ya kazi yake Balozi Dkt. Ezekiel Kyogo ni Amani, Amani, Amani ambayo matunda yake yameonekana kwa kutunukiwa tuzo hiyo ya kipekee ya ubalozi wa Amani Duniani.

SP Balozi Dkt. Ezekiel Kyogo amekuwa na mchango mkubwa katika Taifa wa kuelimisha jamii kuhusu uzalendo na kuhamasisha Amani na hiyo ndiyo kazi yake kubwa anayoifanya ndani ya Jeshi la Polisi kwa liwake jua, inyeshe mvua yeye ni kiguu na njia kwenda kutoa elimu ya kuhamasisha Amani.

Balozi Dkt. Ezekiel Kyogo anasema Tuzo hiyo ya heshima aliyotunukiwa ni ya pili baada ya kutunukiwa ya kwanza Oktoba 17, 2025 na Mufti wa Tanzania Sheikh Dkt. Abubakar Zubeir Bin Ally Temeke Jijini Dar es Salaam.

Balozi Dkt. Kyogo anasema kutokana na majukumu yake ya kazi ya kila  siku ni muelimishaji wa jamii katika masuala ya ulinzi na usalama kwa ujumla wake.

Anasema katika maisha huwezi kuvitenganisha vitu vitatu ambavyo ni Usalama, amani na Utulivu na kueleza kwamba ili kuwepo na utulivu ni lazima kuwepo na usalama, utulivu na ndiyo amani inapatikana.

“Tumekuwa tukivihubiri mara kwa mara kwa jamii kwa muktadha wa kuifanya jamii yenyewe kuwa salama dhidi ya uhalifu lakini kuifanya jamii ya watanzania kuwa salama dhidi ya maadui wa nje na kuifanya kuwa na uzalendo wa nchi yao kuwa salama na utulivu zaidi,” alisema Balozi wa Amani Dkt. Kyogo.

Dkt. Kyogo amesema kazi hiyo wameihubiri katika maeneo mbalimbali ya Tanzania kwa sababu wana amini kwamba amani ikiwepo ndipo maendeleo yanaweza kuwepo, uzalishaji unaweza kuwepo, shughuli za maendeleo zitakuwepo pasipo kuwa na changamoto yoyote.

Anasema kwa ujumla wake ustawi wa binadamu unahitaji  uwepo wa amani na siyo vinginevyo

Dkt. Kyogo anasema kutoweka kwa amani au vurugu anaichukulia kama ni changamoto ya kijamii (Social Probrem) na ili tatizo liwe la kijamii ni lazima liwe lina mgusa kila mtu na likiwa la mtu mmoja haliwezi kuwa la kijamii.

“Linapo mgusa kila mtu, kila sekta na kila mahali linakuwa ni Social Problem na ndiyo maana nikasema kwamba kutoweka kwa amani kwa kuanzisha vurugu linakuwa tatizo la kijamii kwa sababu zinamuathiri kila mmoja wakiwemo wazazi, watoto, walezi, wagonjwa waliopo mahospitali, kundi la watu wasiyojiweza na kuwa vurugu zinapotokea watu hao wanakwenda wapi,” alisema Dkt. Kyogo.

Dkt. Kyogo anasema unapotokea uvunjifu wa amani utatuzi wake unatakiwa uwepo ushiriki wa pamoja wananchi, watu wa makanisa, madhehebu mbalimbali waislamu, wakristo, vijana, wazee kutokana na unyeti wake wa kumgusa kila mmoja.

Aliongeza kuwa ili Taifa liwe salama na uwepo ustawi inatakiwa kukaa pamoja na kuangalia tunatoka vipi kwenye hayo madhira na kwenda kwenye mazingira salama zaidi.

Dkt. Kyogo anasema tangu aanze kufanya kazi hiyo ya kuhamasisha amani ana zaidi ya miaka mitano na kueleza kuwa majukumu ya kuhamasisha amani ni ya kila mtu ingawa baadhi ya watu wanadhani jukumu hilo ni la polisi.

Akizungumzia kutunukiwa tuzo hiyo anasema kimsingi anajisikia furaha na kutambua kwamba kazi anayoifanya mchango wake umeonekana na kwamba mbali ya kufurahi ameongezewa jukumu la kuendelea kuhamasisha amani.

“Ninavyoongea siku hadi siku kuhusu amani bado naona nawiwa kuhamasisha amani ili Tanzania iwe salama  lakini na hata nchi zingine kwa sababu dunia inapokuwa salama  panakuwa mahali sahihi pa kuishi,” anasema Balozi wa Amani Dkt. Ezekiel Kyogo.

Dkt. Kyogo alitumia nafasi hiyo kuyaambia makundi ya vijana na mengine kuwa wanapaswa kuitafakari Tanzania kwa mapana kwamba imejengwa  na imetukuza na kufika hapa tulipo hivyo ni jukumu letu  kuangalia mbinu mbadala na sahihi ya kuiboresha ili twende mbele zaidi  kwa kuitafakari michango yetu ya kuiwezesha kufika mahali inapopaswa kufika.

“Tunatakiwa kuwa na wazo la kuona kwamba sisi kama vijana tutafanya nini kuijenga nchi yetu ifike mahali na kwasabau imefika mahali pazuri hivyo kuna haja ya kuchangia mawazo yetu kusogea mbele zaidi na kuona jinsi gani ya kuifikisha nchi yetu pale wanapoona wanapahitaji,” alisema Dkt. Kyogo.

Katika uelimishaji na uhamasishaji wa amani Balozi Dkt. Kyogo alisema wanalazimika kutumia mbinu mbalimbali zikiwemo adithi ili waeleweke na moja ya adithi yake ni ya kijana Tuntufye.

“ Siku moja watoto wa kijiji kimoja walikaa sehemu na kusemezana wapige kura ili kumpata mama ambaye ni mrembo miongoni mwa mama zao ambapo mtoto aitwaye Isack mama yake aliibuka kidedea kwa kuwa mrembo katika kijiji hicho.

Baada ya kupigwa kura hizo mtoto Isack aliinuka na kutembea kwa madaha akijisifia mbele ya wenzake kuwa mama yake ni mrembo kuliko wakina mama wote pale kijijini.

‘Hapa nazungumzia mapenzi na uzalendo kumbe hata kama mtu hayupo akizungumziwa kwa mema watu wengine wanakuwa na furaha na ndiyo maana mama yake Isack alipotajwa kuwa ni mrembo mtoto wake alijisikia furaha kubwa,” alisema Dkt. Kyogo.

Lakini wakati huohuo watoto hao walisemezana tena kuwa palipo na mrembo hapakosi kuwepo na mwenye sura mbaya, hivyo walipiga kura tena ili kumpata mama mwenye sura mbaya  hapo kijijini kura hiyo ilimuangukia mama yake Tuntufye.

Tuntufye baada ya mama yake kupigiwa kura hiyo moyo wake ulisinyaa, akanung’unika na kuhuzunika. Kumbe kuna uzalendo kati ya mtoto na mama, mama akiguswa kwa ubaya mtoto anasikia maumivu hapa nazungumzia maana ya upendo,’alisema Dkt. Kyogo.

Baada ya mama yake kupigiwa kura hiyo Tuntufye alianza kuondoka kuelekea nyumbani kwao na alipokaribia karibu na mlango wao alimkuta mama yake akiinua mikono na kumkumbatia huku akimuuliza kwa nini analia lakini aliinua uso wake kumuangalia mama yake usoni na kuthibitisha ni kweli alikuwa na sura mbaya.

Tuntufye aliendelea kulia ndipo mama yake alipomkumbatia kwa upendo na kumuambia sikiliza mwanangu “wakati ukiwa mdogo tuliishi kwenye nyumba ya majani moto ulishika ile nyumba ukiwa na miezi miwili mimi mama yako kwa mahaba na upendo wa dhati niliingia ndani kwa ajili ya kukuokoa ndipo moto uliponiangukia usoni na kuharibu sura yangu”.

Baada ya Tuntufye kujua sababu ya mama yake kuwa na sura mbaya alitabasamu hakuhuzunika tena.

Balozi wa Amani Dkt. Kyogo alisema leo hii tungejua Tanzania ilipotutoa na kujengwa kwa jitihada kubwa tungeipenda na kuitunza amani iliyopo kwa kusemezana wenyewe kwa wenyewe ili kuiendeleza na ndiyo maana nimezungumzia dhana nzima ya kushirikiana katika kuijenga amani na nchi yetu ya Tanzania.

“Tanzania inapokuwa na amani hata sisi wana Usalama tuna kuwa tunafanya kazi vizuri na wakati mwingine tunaingia kwenye changamoto mbalimbali kwa kuwa tumekula viapo vya kuhakikisha tunalinda usalama wa raia na mali zao,” alisema Balozi Dkt. Kyogo.

Aidha, Dkt. Kyogo alisema kila mtanzania ana wajibu wa kuilinda amani iliyopo nchini na hakuna mtu wa kuachiwa kuitunza.  

Balozi Dkt. Ezekiel Kyogo akiwa katika moja ya matukio yake ya uelimishaji wa masuala ya kutunza amani
Mrakibu wa Polisi (SP) Balozi Dkt. Ezekiel Kyogo akitoa elimu kuhusu masuala ya utunzaji wa amani.
Balozi Dkt. Ezekiel Kyogo, akisisitiza jambo wakati wa utoaji wa elimu kuhamasisha jamii kutunza amani ya nchi.
Balozi Dkt. Ezekiel Kyogo akiwajibika.
Balozi Dkt. Ezekiel Kyogo (waliosimama nyuma mwenye sare za Polisi) akiwa katika picha na wadau mbalimbali waliotunukiwa tuzo hiyo,

Makala hii imeandaliwa na Dotto Mwaibale simu namba 0754362990 

No comments