Breaking News

NAIBU WAZIRI NDEGE AIPONGEZA SMAUJATA KANDA YA KASKAZINI


Katibu wa  Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania (SMAUJATA) Kanda ya Kaskazinim, Ezekiel Tlanka (katikati), akimkabidhi hati maalumu Naibu Waziri wa Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Manyara (CCM), Regina Ndege kwa kutambua mchango wake. Hafla ya makabidhiano hayo ilifanyika Januari 10, 2026 mkoani Manyara. Kutoka kushoto ni Mwenyekiti Smaujata Wilaya ya Babati, Petro Martin, Naibu Katibu Smaujata Mkoa, Regina Karengi, Mwenyekiti wa Smaujata Mkoa wa Manyara, Hassan Kimu na kulia ni Mkuu wa Idara ya Vijana Smaujata Mkoa, Daniel Damiano. 

....................................

Na Mwandishi Wetu, Manyara
 

Naibu Waziri wa Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Manyara (CCM), Regina Ndege ameipongeza Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania (SMAUJATA), Kanda ya Kaskazini chini ya Katibu wake Ezekiel Tlanka kwa jitihada kubwa wanayoifanya ya kuibua matukio ya ukatili na kuyatafutia ufumbuzi kwa kushirikiana na taasisi zingine likiwemo Jeshi la Polisi.

Mhe. Ndege alitoa pongezi hizo Januari 11, 2026 katika hafla fupi ya kukabidhiwa hati ya shukrani iliyotolewa na Smaujata kanda hiyo kutokana na mchango wake uliofanikisha kikao cha Jumuiya hiyo kilichofanyika Desemba 23, 2025.

“Nimekuwa nikifuatilia utendaji wenu wa kazi na jinsi Smaujata inavyoibua  matukio ya vitendo vya ukatili na kuyafanyia kazi kwa kushirikiana na vyombo vingine likiwemo jeshi letu la Polisi kupitia dawati la jinsia hakika mnafanya kazi kubwa sana ya kuisaidia Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan,” alisema Ndege.

Ndege alitumia nafasi hiyo kuipongeza Smaujata Kanda ya Kaskazini na viongozi wao wote chini ya katibu wake Ezekiel Tlanka na kueleza kuwa kazi wanayoifanya ni ya kujitolea hivyo pindi atakapopata nafasi ataendelea kuwapa msaada.

Aidha, Ndege alisema ataendelea kushirikiana na Smaujata kwa karibu zaidi na kuhakikisha jamii inakuwa salama kwa kuzingatia Mkoa wa Manyara ni miongoni mwa mikoa yenye changamoto ya kuwa na matukio mengi ya ukatili hivyo unahitajika ushirikiano ili kukabiliana na vitendo hivyo na kuhakikisha vinakwisha.

Kwa upande wake Katibu wa Smaujata Kanda ya Kaskazini, Ezekiel Tlanka, alisema mchango wa mbunge huyo unaonesha dhamira ya dhati na vitendo ya kuunga mkono jitihada za Jumuiya hiyo katika mapambano ya vitendo vya ukatili na unyanyasaji hasa katika kanda hiyo.

Tlanka aliomba viongozi wengine kuiga mfano wa kiongozi huyo kwa kujitoa kusaidia jumuiya hiyo ambayo imejikita kupambana na matukio hayo ya ukatili wa kijinsia katika jamii.

Taarifa hii imeandaliwa na Dotto Mwaibale simu namba 0754362990.

Chanzo Smaujata Mkoa wa Manyara.

No comments