Breaking News

RAIS SAMIA: SERIKALI ITAENDELEA KUKABILI UPUNGUFU WA MADAKTARI NCHINI

 

Na Sophia Kingimali. 

Rais Dkt Samia Suluhu Hassan amesema Serikali itaendelea kukabiliana na upungufu wa Madaktari kwani kadri nchi inavyopiga hatua kwenye maendeleo ndivyo uhitaji wa watumishi katika sekta ya afya unavyozidi kuongezeka.

Hayo amesema leo Julai 31,2024 katika kilele cha kongamano ya kumbukizi ya tatu ya Rais Mstaafu wa awamu ya tatu hayati Benjamini Mkapa ambapo kongamano hilo liliandaliwa na Taasisi ya Benjamini Mkapa(BMF).

Amesema Serikali inafahamu umuhimu wa sekta hiyo na inatambua upungufu uliopo hivyo ametoa rai kwa wizara zote ambazo zinahusika na uajili pindi wanapotoa ajira katika sekta waajiri na madaktari wa mkataba ili waweze kujitolea katika hospitali na vituo vya afya vilivyopo nchini.

“Hapa nataka niwe shahidi wa upungufu uliopo kwani ninapozunguka mikoani na wilayani changamoto namba moja ninayokutana nayo ni upungufu wa watumishi katika sekta ya afya na elimu na hii ni kwa sababu ya ongezeko la watu na tunaendelea kuzaliana kila siku kwa hiyo mahitaji ni makubwa na ndio maana kila tunavyoajiri watumishi bado wanakuwa hawatoshi”,Amesema Dkt Samia.

Aidha amesema ajira hizo zinaendana na ukuaji wa uchumi ndio maana inapopatikana nafasi ndogo uchumi ukiongezeka na watumishi sekta ya afya na elimu kunakuwa na upungufu.

Kwa upande wake Waziri wa Afya Ummy Mwalimu amesema miongoni mwa mambo yaliyoibuka kwenye kongamano hilo ni uzalishaji wa madaktari,Wauguzi,wafamasia,wataalamu wa maabara lakini kukosekana kwa ajira kwa wataalam waliopo.

Amesema hivyo miongoni mwa maazimio ni pamoja na kuhakikisha hospitali zinaajili watumishi wa mikataba ambapo mchakato wa bima ya afya kwa wote utakapokamilika utaziwezesha hospitali nchini kuajiri watumishi wa mikataba.

“Madaktari na wataalam tunazalisha wengi kupitia vyuo vyetu nchini na hatuwapi ajira lazima tuangalie namna ya kutatua changamoto hii”,Amesema.

Ameongeza kuwa watakaa na mabaraza ya wanataaluma wakiwemo MAT,wafamasia,wauguzi,maabara ili wakubaliane namna bora ya kudhibiti watumishi wa afya ambao wapo barabarani.

Nae,Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi hiyo(BMF)Dkt Hellen Senkoro amesema katika kipindi cha miaka 18 tangu kuanza kwa taasisi hiyo imeweza kutoa jumla ya ajira 13,000 katika sekta ya afya ambapo zinajumuisha wataalam 7000 wanaojulikana kama Mkapa Fellows na wahudumu ya afya ngazi ngazi ya jamii 6,000.

Ameongeza kuwa pia Taasisi hiyo imetoa ufadhiri wa masomo kwa wanafunzi 1,150 ambao walikwenda vyuoni na kuhitimu katika fani mbalimbali za afya na wengine wanaojiendeleza wakiwa kazini.

No comments