Breaking News

ZOEZI LA UBORESHAJI DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA LATUA SINGIDA, DODOMA

Mjumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama Kuu ya Rufaa, Asina Omari akifungua akifungua mkutano wa Tume na wadau wa uchaguzi kuhusu uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura Mkoa wa Singida Septemba 13, 2024, 

...................................................

Imeandaliwa na Dotto Mwaibale / Solomoni Philemon (0754-362990)


ZOEZI la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ambalo linafanywa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) sasa ni zamu ya Mikoa ya Singida, Manyara na Dodoma.

Akifungua mkutano wa Tume na wadau wa uchaguzi kuhusu uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura Mkoa wa Singida Septemba 13, 2024, Mjumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama Kuu ya Rufaa, Asina Omari alisema maboresho hayo yanakwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia ikiwa ni pamoja na kurahisisha zoezi la uboreshaji wa daftari hilo.

“Tume imeboresha mfumo wa uandikishaji ambao kwa mara ya kwanza utawezesha mpiga kura aliyepo kwenye daftari kuanzisha mchakato wa kuboresha taarifa zake au kuhama kituo kwa kutumia aina zote za simu au kompyuta,” alisema Omari.

Jaji Omari alisema ni kosa la kisheria kwa mtu yeyote kuomba kujiandisha zaidi ya mara moja atakuwa anatenda kosa kisheria ambapo akitiwa hatiani adhabu yake ni faini isiopungua Sh.100,000 na isiyozidi 300,000 au kutumikia kifungo kisichopungua miezi sita na kisichozidi miaka miwili au vyote kwa pamoja.

Mkurugenzi wa  Uchaguzi, Kailima Ramadhani akitoa mada kuhusu uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura alisema kwa kuzingatia matokeo ya Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 jumla ya wapiga kura 5,586,433 wapya wanatarajiwa kuandikishwa ambao ni sawa na asilimia 18.7 ya wapiga kura 29,754,699 waliopo kwenye Daftari baada ya uboreshwaji uliofanyika 2019/ 2020.

Alisema wapiga kura 4,369,531 inatarajiwa wataboresha taarifa zao na wapiga 594,494 inatarajiwa wataondolewa kwenye Daftari kwa kukosa sifa za kuendelea kuwepo kwenye Daftari hilo.

 “ Kwa Mkoa wa Singida Tume inatarajia kuandikisha wapiga kura wapya 216,947 hii ikiwa ni ongezeko la asilimia 26 ya wapiga kura 848,456 waliopo kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura,” alisema Ramadhani.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Daftari na Teknolojia ya Habari (TEHAMA), Stanslaus Mwita alisema katika zoezi la Uboreshaji wa Daftari hilo lililoanza Julai 20, 2024 inatumika mifumo ya aina mbili mfumo mkuu ukiwa ni VRS na mfumo saidizi ukiwa ni OVRS.

Alisema mfumo wa VRS umekuwa ukitumika katika mazoezi ya uboreshaji yote yaliyotangulia (2015 na 2020) na kuwa mfumo wa OVRS ulianzishwa kwa lengo la kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi kwa njia ya mtandao.

Mwita alisema  kwa kutumia Mfumo wa OVRS mpiga kura ili apate taarifa zake anaweza kutumia simu janja, vishikwambi na kompyuta na watahitaji kuwa  na mtandao wa internet ili kupata huduma hiyo ambapo wataingia katika tovuti https://ovrs.inec.go.tz hivyo kupitia anuani hiyo waombaji wataweza kurekebisha taarifa zao, kuhama kituo au kufanya vyote kwa pamoja.

Kwa Mfumo wa VRS unachukua taarifa za miaka ya nyuma kama zilivyo katika fomu za uandikishaji fomu namba 1, 5A,5B na kuwaTaarifa hizo zinahusisha, Taarifa Binafsi za mwombaji, Taarifa za Anuani za makazi na Taarifa za Makazi ya Kudumu na nyingine zote na kuwa Mfumo wa VRS zitatumika Alama za vidole, picha na saini.

Aidha, Mwita alisema Menu Kuu ya kupata taarifa hizo mpiga Kura anatakiwa kupiga *152*00#  na kuwa baada ya hapo atabonyeza namba 8, 2 na 3 na namba nne hapo ataweza kupata taarifa zake.

Akifunga mkutano huo Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) Dkt. Zakia Abubakar, alisema hamasa kubwa ya wananchi kushiriki zoezi la uboreshaji wa Daftari na baadae Uchaguzi litachangiwa na ushirikiano mkubwa zaidi kutoka   kwao kwa kuwafikishia ujumbe huo wananchi.

Dkt. Abubakar alitoa rai kwa washiriki wa mkutano huo kuwaelimisha wanananchi wajue kwamba kujiandikisha au kuboresha taarifa ndio njia pekee itakayowawezesha kushiriki kuwa chagua viongozi wanaowapenda utakapofika wakati wa uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025.

Pia alitumia nafasi hiyo kuwakumbusha washiriki wa mkutano huo kuwa Kaulimbiu ya Uboreshaji wa Daftari hilo kuwa ni “ Kujiandikisha Kuwa Mpiga Kura ni Msingi wa Uchaguzi Bora”

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) ilianza zoezi la uboreshaji wa Daftari hilo baada ya uzinduzi uliofanyika mkoani Kigoma Julai 20, 2024 ambapo mzunguko wa kwanza wa uboreshaji ulifanyika mikoa mitatu ya Kigoma, Tabora na Katavi.

Mzunguko wa pili ulijumuisha mikoa ya Geita na Kagera na mzunguko wa tatu ukiwa ni mikoa ya  Mwanza na Shinyanga, mzunguko wan ne kwenye mikoa ya Mara, Simiyu na Manyara katika Halmshauri ya Wilaya ya Babati, Hanang’, Mbulu na Mji wa Babati.

Aidha, mzunguko wa tano wa uboreshaji wa Daftari hilo utajumuisha Mkoa wa Singida, Mkoa wa Dodoma, Halmashauri za Wilaya ya Bahi, Chamwino na Kongwa na Mkoa wa Manyara katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu na Wilaya ya Kiteto na Simanjirona uboreshaji utaanza Septemba 25, 2024 hadi Oktoba 1, 2024 ambapo vituo vitakuwa vinafunguliwa kuanzia  saa 2:00 na kufungwa saa 12:00 jioni.

Mkurugenzi wa  Uchaguzi, Kailima Ramadhani akitoa mada kuhusu uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.
Mkurugenzi wa Daftari na Teknolojia ya Habari (TEHAMA), Stanslaus Mwita, akitoa mada kwenye mkutano huo.
Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) Dkt. Zakia Abubakar, akifunga mkutano huo.
Kiongozi wa Machifu Mkoa wa Singida Chifu Mughenyi Senge, akichangia jambo kwenye mkutano huo.  
Mwenyekiti wa Vyama vya  Siasa Mkoa wa Singida, Yesaya Mande akichangia jambo kwenye mkutano huo.
Mwenyekiti wa Chama cha SAU Mkoa wa Singida, Hassan Karim akizungumza kwenye mkutano huo.
Viongozi wa dini wakiwa kwenye mkutano huo.
Sheikh wa Mkoa wa Singida, akiwajibika ipasavyo kwenye mkutano huo
Mkurugenzi wa  Uchaguzi, Kailima Ramadhani, akiteta jambo na Mjumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi (INEC), Jaji wa Mahakama Kuu ya Rufaa, Asina Omari ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye mkutano huo.
Washiriki wakiwa kwenye mkutano huo
Viongozi wa vyama vya siasa wakiwa kwenye mkutano huo.
Watu wenye ulemavu wakiwa kwenye mkutano huo.
Mgeni rasmi na viongozi wengine pamoja viongozi wa dini na machifu wakiwa katika picha ya pamoja
Viongozi meza kuu wakiwa katika picha ya pamoja na watu wenye ulemavu.
Viongozi meza kuu wakiwa katikja picha ya pamoja na Wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari
 

No comments