Breaking News

MABONDIA WA MAFIA BOXING PROMOTION WATEMBELEA YATIMA JIJINI TANGA

'Knockout ya Mama' na mgao wa Majiko ya Gesi kwa Mama lishe kwenye masoko Tanga.

 


Msaada wa vyakula ukitolewa kwa Yatima Mkoa wa Tanga

 

Na Mashaka Kibaya, Tanga

............................. 

MABINGWA wa Masumbwi katika mapambano ya 'Knockout ya Mama' Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, wamerejesha fadhila kwa jamii baada ya kuamua kugawana sehemu ya walichokipata kufuatia ushindi mkubwa  kwenye mpambano wao wa ngumi ulifanyika hivi karibuni.

Mabondia hao kutoka Kampuni ya Mafia Boxing Promotion wametua Jijini Tanga baada ya mapambano yao Jijini Dar es Salaam ambapo walitembelea Kituo cha kulelea Watoto Yatima pia walikutana na mama lishe kwenye masoko.

Katika Kituo cha kulelea Watoto Yatima cha Green Cresent Foundation timu hiyo ya mabondia na Uongozi wa Mafia Boxing Promotion waligawa vyakula,vinywaji laini na majiko ya gesi, misaada ambayo iliibua faraja kwa walengwa na wasaidizi wao.

Mbali na kutoa misaada hiyo kwa kundi hilo la Yatima lenye Makao yake Mitaa ya Bombo Jijini Tanga, lakini pia mabondia hao walitembelea Masoko ya Makorora, Mgandini na Mlango wa Chuma kote wakigawa Majiko ya Gesi kwa Mama lishe.

Lengo la ugawaji wa Majiko hayo ya Gesi ni ili kuleta mabadiliko chanya kwa Wajasiriamali hao kuondokana na matumizi ya kuni na Mkaa na hivyo kupunguza vitendo vya uharibifu wa mazingira.

Katika mazungumzo yake kwenye ziara hiyo, Mkurugenzi Mkuu Matangazo na Uzalishaji, Omari Clayton alisema,ushindi huo wa mabondia hao Vijana wa Kitanzania kutoka Mafia Boxing Promotion ni matokeo ya hamasa kubwa kutoka kwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan.

Clayton alisema ahadi ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa Vijana iliamsha ari,chachu na motisha kubwa ya ushindi kwa mabondia hadi  kuweza kufanikiwa kunyakuwa mikanda yote iliyoshindaniwa.

"Baada ya Mama (Rais) kuwaahidi Vijana nao wakapata ari ya kufanya vizuri kama ilivyo kwenye mpira wa miguu...sasa kile walichokipata wakasema hapana tuna wadogo zetu mayatima na hata mama lishe tukashiriki nao" alisema Omari Clayton.

Kapteni wa mabondia hao Ibrahim Mustafa mshiriki na Mshindi wa WBC Afrika alielezea faraja yake baada ya wao kufanikiwa kupeperusha vyema bendera ya Tanzania ambapo alimshukuru Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa mchango wake kwenye medani hiyo ya mchezo wa ngumi.

Aidha bondia huyo alisema kwamba,katika mapambano ya 'Knockout ya Mama' licha ya hamasa waliyoipata kutoka kwa Rais pia wanaamini kuwa Watanzania wakiwemo Yatima na wapenzi wa michezo waliwaombea kwa Mungu na ndio sababu na wao wakaona vyema kuungana nao.

Bi. Zainati Saidi ni Mama Mlezi wa Kituo cha Yatima cha Green Cresent Foundation, amewashukuru Mafia Boxing Promotion kwa misaada waliyowapatia huku akiungana na watoto Yatima waliokuwepo kuwaombea Mungu mabondia kuendelea kufanya vizuri.

Vilevile kwa upande wa Mama lishe waliopatiwa majiko ya Gesi waliwasilisha Shukrani zao kwa mabondia wa Mafia Boxing Promotion na Serikali ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuwapatia vitendea kazi hivyo wakiamini kuwa vitawasaidia katika kuimarisha utendaji kazi wao.


Msaada ukitolewa.

 

No comments