Breaking News

DEREVA NA KONDAKTA WAKE WADAKWA NA POLISI WAKISAFIRISHA DAWA ZA KULEVYA

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP ), Almachius Mchunguzi akizungumza na waandishi kuhusu kukamatwa kwa watuhumiwa hao pamoja na dawa hizo za kulevya.

.......................................

Na Mashaka Kibaya, Tanga

WATU wawili akiwemo Dereva Hashimu Juma Mohamed (46) na Kondakta Ramadhani Ismail Mbaruku (28) wanashikiliwa na Polisi mkoani Tanga wakituhumiwa kusafirisha dawa za kulevya 'Mirungi' kwa kutumia gari lenye namba za usajili T 689 EJJ aina ya Coaster Hino.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Kamishna Msaidizi  wa Polisi (ACP) Almachius Mchunguzi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo katika taarifa yake aliyoitoa Jana kwa Waandishi wa habari Ofisini kwake Jijini Tanga.

Kukamatwa kwa watuhumiwa hao ni matokeo ya msako uliofanywa na Polisi Disemba 10 mwaka huu huko Kijiji cha Makuyuni tarafa ya Mombo Wilayani Korogwe, watu hao walikamatwa wakitokea Mkoani Kilimanjaro kuelekea katika jiji la Dar es Salaam.

ACP Mchunguzi alisema, katika upekuzi wa gari watuhumiwa walikutwa na Mirungi bunda 962 sawa na Kg 411.05 dawa ambazo zilikuwa zukisafirishwa kwa lengo la kuingizwa Sokoni.

Watuhumiwa watafikishwa Mahakamani wakati wowote baada ya taratibu za kisheria kukamilika huku Kamanda Mchunguzi akiweka bayana baadhi ya mafanikio waliyoyapata kwa kipindi cha Nov hadi Disemba 2024.

Alisema,kwa upande wa kesi zilizofikishwa Mahakamani mwezi Novemba hadi Disemba 2024 watuhumiwa wanne wamehukumiwa vifungo vya maisha na wengine watatu wamehukumiwa kwenda jela kutumikia kifungo miaka 30.

Amemtaja Mwamini Mgeja (32) mkulima na mkazi wa Kilindi Asilia kuhukumiwa kifungo cha maisha jela kwa kosa la kumbaka mtoto wake wa kambo mwenye Umri wa miaka tisa (9) na Jonas Alphan (38) mkulima na mkazi wa Gombero Kilindi aliyehukumiwa kifungo cha maisha jela kwa kosa la kumbaka mtoto wa miaka 4.

Mwingine aliyehukumiwa kifungo cha maisha jela ni Rajabu Juma , mkulima na mkazi wa Mafleta Kilindi baada ya kupatikana na hatia ya kumbaka mtoto wa miaka 17 huku Salimu Riziki na Athuman Salumu Jumaa wakihukumiwa kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la unyany'anyi wa kutumia silaha na miaka 20 jela kwa kosa la kumiliki silaha kinyume cha Sheria.

Pia Richard Kiwango Shelukindo (45) mkulima na mkazi wa Kwaludege Handeni amehukumiwa kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la kulawiti mtoto wa miaka 5 na Mansuri Omari (19) mkulima na mkazi wa Kwakibuyu Pangani amehukumiwa kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la kumbaka binti mwenye Umri wa miaka 16.

Wito umetolewa na Jeshi la Polisi Mkoani Tanga kwa wananchi wote kuelekea msimu wa Sikukuu za mwisho wa mwaka Krismasi na mwaka mpya ,Madereva kuzingatia Sheria za Usalama barabarani kuepuka mwendo Kasi ,ulevi wakati wa kuendesha magari.

Aidha Kamanda Mchunguzi amewataka Wananchi wote kuzingatia kanuni,sheria na taratibu za kudumisha Amani na Usalama wa Mkoa wa Tanga. 

No comments