Breaking News

WANACHUO TANGA MBARONI KWA KUHUSISHWA NA WIZI WA KIMTANDAO

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP ), Almachius Mchunguzi akizungumza na waandishi kuhusu tukio hilo.

............................

Na Mashaka Kibaya, Tanga 

MWANAFUNZI wa Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) Peter Michael Babuya (24) na wenzake wengine watano wanashikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoani Tanga wakituhumiwa na makosa ya Wizi kwa njia ya Mtandao.

Wengine wanaoshikiliwa pamoja na Mwanafunzi huyo ni Said Amiri 'Mofisamchayungu' (21) mkazi wa Kimara Dar es Salaam, Athumani Amiri Athumani (24) mkazi wa Mbezi mwisho Dar es Salaam.

Pia wamo Brayani Matina Mayunga 'Festo Madenge' (26) mkazi wa Mombasa Ukonga Dar es Salaam na Wakala James John Nathaniel (24) mkazi wa Kitunda Dar es Salaam.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga ACP Almachius Mchunguzi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo akisema, watuhumiwa hao wamekamatwa kwa nyakati tofauti katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

Alisema,Watuhumiwa hao wamekuwa wakijifanya mawakala wa kujitegemea (Freelancers) wa Kampuni za Tigo, Vodacom na Airtel na kuiba fedha kiasi cha Shilingi 20,390,000 (Milioni Ishirini na laki tatu na tisini elfu) kwa njia ya Mtandao Mali ya Abdul Hemed Shedafa mfanyabiashara na mkazi wa Muheza Mkoani Tanga.

Kwa mujibu wa Jeshi la Polisi baada ya uchunguzi wa kitaalamu kufanyika ndipo ilipobainika kuwa Watuhumiwa walitumia mbinu za udanganyifu ikiwemo kutumia namba za simu zilizosajiliwa kwa majina mengine ili kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.

Kwa upande wa makosa ya Usalama barabarani ACP Mchunguzi alisema, Madereva 56 wameondolewa madaraja na kufungiwa leseni zao kwa muda kutokana na makosa mbalimbali ya barabarani na wengine wakilipa faini Mahakamani kwa makosa ya ukiukaji wa Sheria za Usalama barabarani.

Aidha kwa kipindi cha Novemba hadi Disemba 18,2024 Jeshi la Polisi Mkoani Tanga katika operesheni zake za kuimarisha doria na misako imewakamata Watuhumiwa 95 wakiwa na makosa mbalimbali ukiwemo uvunjaji,kujeruhi,wahamiaji haramu na kupatikana na dawa za kulevya .

Katika kudhibiti matukizi ya dawa za kulevya kwa kipindi cha Novemba hadi Disemba 2024 Polisi umekamata dawa za kulevya aina ya Mirungi Kg 529 .49 ,bhangi Kg 563, na Pombe ya Moshi Lita 179.5.

Vilevile wahamiaji haramu watatu kutoka nchini Ethiopia wamekamatwa, mali mbalimbali za wizi ikiwa ni pamoja na televisheni 10 aina mbalimbali, pikipiki Sita aina mbalimbali,fridge mbili aina ya Rock rangi nyeupe, simu 30 za smart phone na simu ndogo 07,na madumu ya mafuta ya Kula 864 yaliyoingizwa kwa njia ya magendo ikiwa ni pamoja na kukamatwa kwa watuhumiwa wa matukio hayo.

Jeshi la Polisi Mkoani Tanga linatoa onyo kwa wananchi wote wanaojishughulisha na makosa ya jinai na makosa ya kimtandao kuwa hawataachwa salama bila kuchukuliwa hatua kali za kisheria.

No comments