Breaking News

POLISI KANDA MAALUMU YA DAR ES SALAAM KUENDELEA KUSHIRIKIANA NA WANANCHI KUKOMESHA UHALIFU

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Muliro Jumanne Muliro akitoa taarifa ya matukio mbalimbali ya uhalifu yaliyofanyika wakati wa sherehe za Krisimasi na Mwaka Mpya.

.......................................

 

Na Dotto Mwaibale, Dar es Salaam

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam litaendelea kushirikiana na wananchi ili kuimarisha mifumo ya ulinzi shirikishi kwa ajili ya kupata taarifa mbalimbali za kihalifu na kuwabaini watuhumiwa sanjari na kuwakamata.

Akizungumza na waandishi wa habari Januari 2, 2025 Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Muliro Jumanne Muliro wakati akitoa taarifa ya matukio ya uhalifu na madereva kuendesha vyombo vya moto wakiwa wamelewa katika  kusherehekea sikukuu za krisimasi na mwaka mpya alisema mafanikio hayo waliyoyapata yametokana na ulinzi shirikishi.

Alisema jeshi hilo Kanda Maalum ya Dar es Salaam limewafungia leseni za udereva madereva kadhaa waliokamatwa wakiendesha magari yao huku wakiwa na kiwango kikubwa cha ulevi jambo ambalo ni kosa kisheria.

Alisema madereva hao wamefungiwa kuendesha magari kwa muda wa miezi sita na kuwa hatua hiyo ni kwa mujibu wa kifungu 28 (3) (b) cha Sheria ya Usalama Barabarani Sura 168 iliyofanyiwa marekebisho Mwaka 2002.

"Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam katika kusherehekea Krismasi na Mwaka Mpya tulijipanga vizuri na kuweka usimamizi madhubuti wa Sheria na kanuni mbalimbali zikiwemo za usalama barabarani ili kudhibiti ajali za barabarani," alisema Muliro.

Muliro alitaja makosa hatarishi ambayo yangepelekea ajali yalidhibitiwa na kuchukiliwa hatua kwa wahusika ambapo jumla ya madereva 179 walipimwa ulevi kati yao madereva 30 walikutwa na ulevi wa kiwango cha zaidi ya milligramu 80.

Alisema madereva 22 walikamatwa Wilaya ya Kinondoni, Madereva sita (6) Wilaya ya Ilala na madereva wawili (2) Wilaya ya Temeke.

SACP Muliro alisema katika kipindi cha Novemba hadi Desemba 2024, Jehi hilo lilifanikiwa kupata matokeo mahakamani ya watuhumiwa mbalimbali ambapo Sadick Foreni (30) mkazi wa Mbagala katika Mahakama ya Wilaya ya Temeke alihukumiwa kifungo cha maisha jela kwa kosa la kulawiti huku Joseph Ferdinand (35) mkazi wa Mbagala Kibonde Maji akifungwa  maisha jela kwa kosa la kulawiti.

SACP Muliro amebainisha kuwa, Ayub Hatibu (32) mkazi wa Tabata alihukumiwa na Mahakama ya Wilaya ya Kinyerezi  miaka 30 jela kosa la kubaka huku Salmin Athuman (30) makazi wa Kitunda akihukumiwa kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la unyang'anyi wa kutumia silaha.

Ameongeza Henry Peter (36) mkazi wa Mezi alihukumiwa na Mahakama ya Wilaya ya Ubungo miaka 30 jela kwa kosa la kubaka huku Ramadhan Amir (30) mkazi wa Kawe akihukumiwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinondoni kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la unyang'anyi wa kutumia silaha.

Aidha, Kamanda Muliro alisema jumla ya watuhumiwa 250 walikamatwa kwa kuhusika na kuuza, kusafirisha na kutumia Dawa za Kulevya.

Katika mkutano huo na waandishi wa habari Elizabeth Pascal mkazi wa Kipunguni Mashariki Kata ya Ukonga na Patrick Emmanuel walipata fursa ya kutoa ushuhuda wa jinsi jeshi hilo la Polisi Kanda ya Dar es Salaam walivyofanikiwa kukamata vifaa vyao vilivyokuwa vimeibwa kwenye nyumba zao pamoja na wahusika.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Muliro Jumanne Muliro akionesha waandishi wa habari moja ya TV iliyokamatwa baada ya kuibiwa.
Waandishi wa habari wakichukua taarifa hiyo.
 

No comments