TMA YATOA TAHADHARI KWA WANANCHI KIPINDI CHA JUNI HADI AGOSTI 2025
.......................................
Na Dotto Mwaibale, Dar es Salaam
MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania(TMA) imetoa
ushauri kwa wananchi kuchukua
tahadhari za kiafya katika kipindi cha mwezi cha Juni hadi Agosti ambacho kitatawaliwa na hali ya baridi.
Tahadhari hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mkuu wa
TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya hali
ya hewa na tabia nchi Dkt. Ladslaus Chang’a wakati akizungumza na waandishi wa
habari Jijini Dar es Salaam Mei 22, 2025 ambapo alihimiza wadau mbalimbali watumie
taarifa za hali ya hewa katika utekelezaji wa majukumu yao kwa kipindi cha Juni
hadi Agosti kutokana na kutawaliwa na hali
ya baridi.
“
Kipindi hicho maeneo mengi yanatarajiwa kupata baridi kali na vumbi hivyo wafugaji
wanashauriwa kuzingatia ratiba za kuogesha mifugo na kufuata ushauri wa
wataalamu, huku wakulima wakihimizwa kutumia maeneo oevu kwa kilimo cha mazao
ya muda mfupi kama mbogamboga na viazi,” alisema.
Aidha, alisema watumiaji wa shughuli za baharini wanatakiwa kufuatilia utabiri
wa kila siku na angalizo kuhusu upepo mkali kwa usalama wao.
Akizungumzia msimu huo Chang’a alisema hali ya baridi ya wastani hadi joto
kiasi inatarajiwa katika maeneo mengi ya nchi na kuwa hali ya baridi ya
wastani hadi baridi kali inatarajiwa katika maeneo ya mikoa ya Kigoma, Tabora,
Katavi, Rukwa, Singida pamoja na maeneo ya magharibi mwa mkoa wa Dodoma.
Alisema mwezi Julai ndio kipindi cha baridi
zaidi, huku maeneo yenye miinuko ikitarajiwa kushuka chini ya nyuzi joto 6°C,
hasa katika nyanda za juu kusini-magharibi.
Aidha amesema vipindi vya baridi zaidi
vinatarajiwa kujitokeza katika mwezi Julai na vipindi vya mvua za nje ya msimu
vinatarajiwa katika maeneo ya ukanda wa Ziwa Victoria, ukanda wa mwambao wa
pwani pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba.
Amesema msimu wa kipupwe 2025 unatarajiwa
kutawaliwa na upepo wa wastani utakaovuma kutoka kusini Mashariki kwa maeneo
mengi ya nchi, na vipindi vichache vya upepo mkali utakaovuma kutoka kusini
(upepo wa kusi) hususan katika kipindi cha miezi ya Juni na Julai 2025 katika
maeneo ya ukanda wa pwani ya Bahari ya Hindi na maeneo ya nchi kavu.
TMA imetabiri upepo wa wastani kutoka Kusini Mashariki
utakaotawala maeneo mengi, huku vipindi vya upepo mkali kutoka kusini (upepo wa
kusi) vikitarajiwa hususan mwezi Juni na Julai, hasa katika ukanda wa pwani ya
Bahari ya Hindi na baadhi ya maeneo ya nchi kavu.
Mwelekeo wa Mifumo ya Hali ya Hewa
Kwa mujibu wa TMA, joto la bahari linatarajiwa kuwa la wastani katika maeneo
mengi ya tropiki, huku joto la juu ya wastani katika eneo la kusini magharibi
mwa Bahari ya Hindi likitarajiwa kudhoofisha upepo wa baridi kutoka kusini.
Angalizo
TMA itaendelea kufuatilia hali ya hewa na kutoa taarifa za mara kwa mara.
Wananchi na wadau wanahimizwa kufuatilia utabiri wa saa 24, siku 10 na mwezi
kutoka TMA pamoja na tahadhari zinazotolewa kuhusu hali mbaya ya hewa.
Kwa taarifa zaidi, tembelea tma.go.tz au akaunti rasmi za TMA katika mitandao
ya kijamii.
Post Comment
No comments