Breaking News

AHADI HEWA ZA VIONGOZI ZAWACHOSHA WANANCHI KIVULE, MSONGOLA

Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, Ojambi Masaburi akizungumza kwenye mkutano mkuu wa Umoja wa Litongo Dar es Salaam (ULIDA) ambapo pia alitoa ufafanuzi wa utekelezaji wa miradi ya barabara katika maeneo ya Kata za Msongola na Kivule.

...............................

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam 

WANANCHI wa Kata ya Msongola na Kivule Ilala Jijini Dar es Salaam wamesema wamechoshwa na ahadi ambazo zimekuwa zikidaiwa kutolewa na viongozi mbalimbali wa Serikali kuhusu ujenzi  wa miundombinu ya barabara.

Watetoa malalamiko hayo kwa nyakati tofauti wakati wakizungumza na waandishi wa habari kuhusu kadhia wanayoipata hasa katika kipindi hiki cha mvua aza masika zinazoendelea kunyesha.

Mkazi wa Msongola Colman Marwa ambaye ni Mwenyekiti Mstaafu wa Mtaa wa Yangeyange alisema changamoto ya barabara ni ya muda mrefu hivyo anaiomba Serikali kusikia kilio cha wananchi juu ya ujenzi wa barabara hizo.

“Mimi nipo katika eneo ili tangu mwaka 2000 naona barabara ya kutoka njia panda ya Kivule hadi Kitunda na kipande cha barabara kutoka Msongola hadi Mbande jinsi ambavyo viongozi wamekuwa wakitoa ahadi za kuzitengeneza lakini hatuoni matokea,” alisema Marwa.

Alisema hata mwaka huu barabara hizo zilianza kutengenezwa lakini zimekuwa hazikamiliki huku kizingizio kikubwa ikiwa ni mvua jambo ambalo limewafanya wananchi wakosema Imani na ahadi hizo zinazotolewa na viongozi hao.

Mkazi wa Msongola kwa Chande,  Hadija Rajabu alisema kutokana na ubovu huo wa barabara wanalazimika kulipa nauli mara mbili au zaidi ile ya kawaida.

“ Kutokana na ubovu wa barabara dereva wa bajaji au bodaboda anapandisha nauli anayoitaka mfano sehemu tunayopaswa kulipa nauli ya Sh. 500 kwa bajaji kutoka Njia Panda ya Kivule hadi Fremu Kumi tunatozwa Sh.1000 hadi 1500,” alisema.

Aliongeza kuwa athari wanazokumbana nao ni wajawazito kuwa katika wakati mgumu wanapokwenda Hospitali ya Wilaya ya Kivule kujifungua kutokana na kurushwarushwa kutokana na ubovu huo wa barabara.

Mkazi wa Msongola ambaye ni dereva wa bodaboda Omari Jafari alisema yupo katika eneo hilo tangu 2015 na katika kipindi cha Rais wa Awamu ya Tano Hayati John Pombe Magufuli aliagiza barabara hizo zikiwekwa kifusi ikiwa ni maandalizi ya kujengwa kwa kiwango cha lami lakini mpaka leo hii kipande cha barabara kutoka Msongola hadi Mbande kina hali mbaya na magari yanapita kwa kushida kutoka na mashimo makubwa na madimbwi ya maji.

Mkazi wa Yangeyange Waitara Magori alisema kutokana na ubovu wa barabara hizo sehemu ambayo walipaswa kutumia kwa dakika tano hadi hadi kumi wanatumia zaidi ya nusu saa hadi saa moja.

Dereva bodaboda, Dismas James mkazi wa Kivule anasema kutokana na ubovu wa barabara hizo ameathirika kiafya kwani  amekuwa akipata maumivu ya mgongo.

Diwani wa Kata ya Msongola, Azizi Mwalile alikiri kuwepo kwa changamoto ya barabara hizo na kueleza kwamba tayari Serikali imeanza kuzifanyia kazi akitolea mfano ya barabara ya kutoka Msongola kwenda Kivule imeanza kujengwa na mkandarasi wa Kampuni ya Jiangxi Geo Engineering ya China kupitia mradi wa DMDP-2.

Kwa upande wake Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, Ojambi Masaburi alisema ni kweli hali ya barabara hizo sio nzuri lakini Serikali imeanza kuzifanyia kazi barabara hizo na wakandarasi wapo kwenye maeneo ya mradi baada ya kusaini mkataba wa ujenzi.

“Changamoto iliyopo hivi sasa ni hizi mvua zinazoendelea kunyesha zinawapa wakati mgumu wakandarasi na kushindwa kufanya kazi,” alisema Masaburi.

Masaburi alitumia nafasi hiyo kumshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha za ujenzi wa barabara hizo ambapo amewaomba wananchi kuendelea kuwa na subira.

Diwani wa Kata ya Msongola, Azizi Mwalile akizungumzia hatua iliyochukuliwa na Serikali na kuanza kuzijenga barabara hizo.
Mtambo wa kutengeneza barabara wa Kampuni ya Jiangxi Geo Engineering ya China ukichimba mtaro katika barabara ya Msongola kwenda Kivule kama ulivyonaswa na kamera yetu.
Mkazi wa Msongola kwa Chande,  Hadija Rajabu, akizungumzia adha wanayoipata kutokana na uchakavu wa barabara.
Muonekano wa madimbwi ya maji katika barabara hiyo.

Mkazi wa Yangeyange Waitara Magori, akizungumzia kero za barabara hizo.
Dereva bodaboda, Dismas James, akizungumzia kero ya barabara hiyo.




Muonekano wa uchakavu wa barabara hizo.
 

No comments