Breaking News

MTOTO ANAYESUMBULIWA PUMU YA NGOZI NA MOYO MAISHA YAKE HATARINI

AOMBA MSAADA WA MILIONI TATU ZA MATIBABU

Hali ilivyo hivi sasa ya Mtoto Abubakar Tenda (10) anayesumbuliwa na maradhi ya pumu ya ngozi na moyo kwa zaidi ya miaka tisa.

........................................
 

Na Dotto Mwaibale, Dar es Salaam

MAISHA ya Mtoto Abubakar Rajab Tenda (10) ambaye kwa zaidi ya miaka tisa hajawahi kufurahia maisha  na kuwa mdhoofu wakati wote kutokana na maradhi ya moyo na pumu ya ngozi yanayomsumbua maisha yake yapo hatarini kwa kukosa Sh. Milioni 3.2 za matibabu hivyo anaendelea kuwaomba watanzania wamsaidie.

Mama ya mtoto huyo Latifa Saidi (37) mkazi wa Mtoni Mtongani jirani na Msikiti Mweupe Mtaa wa Mseti Temeke Jijini Dar es Salaam anasema hana fedha za matibabu ya mwanaye huyo ambaye wakati wote iwe mchana, iwe usiku amekuwa  akijikuna kwa kutokwa upele mithiri ya magamba ya samaki huku akipata maumivu makali.

“Tumaini langu la kupata matibabu ya Abubakar nawaachia watanzania kwani ndani ya kipindi cha miaka tisa  nimekuwa nikiangaika naye sehemu mbalimbali kwa ajili ya matibabu nimeshindwa kupata kiasi hicho cha fedha kama nilivyoambiwa na daktari wake,” alisema Latifa.

Latifa anasema mtoto huyo hajawahi kupata usingizi na kuwafanya wawe wanakesha wakimuangalia jinsi anavyojikuna na kuugulia maumivu.

Mama huyo anasema alimzaa Abubakar Juni 10, 2014 Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Temeke Jijini Dar es Salaam akiwa na kilo 4.5 na kuwa alianza kuona mabadiliko ya mtoto wake alipofikisha miaka mitatu kwani ngozi yake ilianza kuonesha kutokwa na upele ndipo alipo mpeleka Hospitali ya Bruda iliyopo Kijichi lakini hakupata nafuu.

Latifa anasema aliendelea kumtibu katika hospitali mbalimbali na alipofikisha miaka sita akawa anapata joto kali nyakati za usiku, kukooa na uso kuvimba ndipo alipompeleka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Temeke walimuambia alikuwa na changamoto ya moyo hivyo ampeleke Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) kwa ajili ya matibabu.

Alisema baada ya kufanyiwa vipimo alielezwa kuwa moyo wake umetanuka hivyo anatakiwa kufanyiwa upasuaji kwa gharama ya Sh. Milioni 3.2 fedha ambazo ameshindwa kuzipata jambo linalomfanya mtoto wake huyo aendelee kuteseka na kushindwa kuanza shule.

“Kwa kweli sijui hatima ya mwanangu kwani wakati wote hana furaha na sijui nitapata wapi hizo fedha sina na  mume wangu naye hana kazi ya uhakika hivyo kutuwia vigumu namna ya kupata fedha hizo,” alisema Latifa.

Alisema mwezi uliopita ndio ilikuwa ampeleke kliniki lakini hadi leo hii ameshindwa kufanya hivyo kwani kila inapofika tarehe ya kliniki anatakiwa awe na Sh. 120,000 kwa ajili ya vipimo na mahitaji mengine ya chakula na usafiri fedha ambayo hana kwani hata kodi ya nyumba ambayo ni zaidi ya Sh.250,000 ameshindwa kulipa hivyo ametakiwa aondoke kwenye nyumba hiyo na kumfanya hazidi kuchanganyikiwa na kuona dunia kama imemtupa.

“Sina mbele wala nyuma sijui nitazimaliza vipi hizi changamoto nilizonazo nawaombeni watanzania wenzangu kwa umoja wenu mnisaidie matibabu ya mtoto wangu,” alisema Latifa akionesha kukata tamaa kabisa ya maisha.

Ndugu zangu watanzania mmeyasikia madhira yanayomsibu mtoto huyo pamoja na changamoto alizonazo mama yake Latifa Saidi anaomba msaada wetu kwa chochote kile utakachoweza kumsaidia kwake kitakuwa ni kikubwa kwani kuna usemi wa Kiswahili unaosema haba na haba ujaza kibaba lengo ni zipatikane fedha za matibabu ya mtoto wake huyo.

Kwa atakaye kuwa tayari kumsaidia mtoto huyo hata kwa Sh. 2000 ana weza kuwasiliana na mama yake  moja kwa moja kwa namba ya simu 0788034472 au Mwandishi wa taarifa hii kwa namba 0754362990.

Taarifa hii nimelazimika kuirudia kuiandika kwa mara ya pili baada ya Juni 6, 2025 kwenda kumjulia hali mtoto huyo na kumkuta akiwa katika hali isiyoridhisha kwani hivi sasa anashindwa kutembea vizuri huku upele ukiendelea kusambaa mwili mzima na mapigo ya moyo yakipanda kwa nguvu, shime watanzania kila mmoja kwa uwezo na imani yake tuungane kwa pamoja kuokoa maisha ya mtoto huyu anayepitia wakati mgumu kwa kukosa Sh. Milioni 3.2 za matibabu.

Hali ilivyo ya mtoto Abubakar

Latifa Said, akiwa na mtoto wake nyumbani kwao wanakoishi Mtoni Mtongani

No comments