Breaking News

MWANGI ACHUKUA FOMU KUWANIA UDIWANI KATA YA IPEMBE MANISPAA YA SINGIDA

ATAJA BAADHI YA VIPAUMBELE VYAKE 
 Mwalimu Gabriel Gunda akimkabidhi fomu Omari Hamisi Mwangi (kulia), ya kugombea udiwani Kata ya Ipembe Manispaa ya Singida kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM). Makabidhiano hayo yamefanyika leo Agosti 18, 2025.
................................................

Na Dotto Mwaibale, Singida

HALMASHAURI Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mkoa wa Singida imemteua kada wa chama hicho Omari Hamisi Mwangi kuwa mgombea wa udiwani wa Kata ya Ipembe ambayo hiyo Manispaa ya Singida.

Mwangi leo Agosti 18, 2025 amekabidhiwa fomu ya kuwania nafasi hiyo ambapo atapambana na wagombea wa vyama vingine kuwania nafasi hiyo katika kata hiyo.

Katika kura za maoni zilizopigwa na wajumbe wa CCM wa kata hiyo Mwangi  aliibuka kidedea kwa kupata kura 86 dhidi ya Mohammed Ali ambaye alipata kura 34, Said Abdallah ambaye alipata kura 6 na Mwanahamisi Juma aliye ambulia kura 4.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kukabidhiwa fomu hiyo alitaja baadhi ya vipaumbele vyake iwapo atashinda nafasi hiyo kuwa atatenga ratiba ya kufanya mikutano na waananchi ili kujua changamoto zao ili kuzitafutia ufumbuzi wa pamoja.

“Nitafufua utaratibu wa kufanya mikutano ya mara kwa mara na wananchi ili kusikiliza changamoto zao na kuzitafutia ufumbuzi kwa pamoja  na zile ambazo zitakuwa nje ya uwezo wangu nitaziwasilisha ngazi ya juu kwa hatua ya utekelezaji,” alisema Mwangi huku akishangiliwa na baadhi ya watu waliomsindikiza kuchukua fomu.

 Alisema iwapo atashinda katika kinyanganyiro hicho atahakikisha anashirikiana na wananchi wote kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo na kuinadi ilani ya uchaguzi ya CCM ya 2025/ 2030.

Wakati huo huo Mwangi amewataka wananchi na wana CCM kujitokeza kwa wingi kushiriki kikamilifu kupiga kura katika Uchaguzi mkuu wa 2025 na kuhakikisha wanawachagua wagombea wote wanaotokana na CCM Kuanzia Diwani, Mbunge na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Taifa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

“Siku ya kupiga kura tukapige kura nyingi kwa wagombea wa CCM jambo ambalo litamsaidia Rais atakayetokana na CCM kufanya kazi yake kwa wepesi,” alisema Mwangi. 

Mwangi mpaka anachaguliwa kuwa mgombea   wa nafasi hiyo amekuwa akihudumu nafasi ya Katibu wa Hamasa wa CCM Kata ya Ipembe.

Omari Hamisi Mwangi akiwa kwenye gari rasmi huku akipeperusha bendera wakati akienda kuchukua fomu.
Hivi ndivyo alivyosindikizwa na makada wa CCM kwenda kuchukua fomu.
Taswira ya msafara wakati wa kwenda kuchukua fomu.
Omari Hamisi Mwangi akionesha fomu baada ya kukabidhiwa.
 

No comments