Breaking News

KAMPUNI ZA DNATA, EMIRATES LEISURE RETAIL ZANZIBAR ZAFANYA USAFI UFUKWENI

Wafanyakazi wa Kampuni za  Dnata na Emirates Leisure Retail Zanzibar wakifanya usafi wa  mazingira katika Ufukwe wa Buyu uliopo Chukwani Zanzibar Septemba 18, 2025.

......................................

Na Dotto Mwaibale, Zanzibar

KAMPUNI za  Dnata na Emirates Leisure Retail Zanzibar zimeendelea kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi za utunzaji wa mazingira kwa kufanya usafi wa Ufukwe wa Buyu uliopo Chukwani.

Katika muendelezo wa kuungamkono jitihada hizo za Serikali za uhifadhi na utunzaji wa mazingira leo Septemba 18, 2025 ‎kampuni hizo zimeshirikiana kufanya kazi hiyo katika ufukwe huo.

Afisa Utawala Msaidizi wa Kampuni ya Emirates Leisure Retail Zanzibar, Ramadhan Hussein Layya (Maarufu Msokolo), akizungumza na waandishi wa habari alisema kampuni hizo zimekuwa na utaratibu wa kushirikiana katika mambo mengi likiwemo la kufanya usafi.

“Kazi hii ya utunzaji wa mazingira kwa kufanya usafi makampuni yetu yamekuwa yakishirikiana na kwetu jambo la utunzaji wa mazingira ni endelevu na siyo la Serikali pekee ndiyo maana tunaiunga mkono,” alisema Msokolo.

‎Alisema zoezi hilo la kufanya usafi halikulenga kuondoa takataka tu katika ufukwe huo, bali kuchukua jukumu la kulinda mazingira, kuhifadhi viumbe wa baharini, na kuhakikisha urembo wa asili wa Zanzibar unabaki salama kwa vizazi vijavyo.‎‎

‎ Msokolo alisema zaidi ya wafanyakazi 50 kutoka katika kampuni hizo walishiriki katika kazi hiyo ya kufanya usafi ambapo waliweza kukusanya kilo 1,000 za chupa za plastiki na taka mbalimbali kutoka ufukweni na chini ya bahari.

“ Kila chupa iliyokusanywa kwetu imekuwa ni hatua moja ya kusonga mbele kuelekea bahari safi na sayari yenye afya,” alisema Msokolo.‎

‎Alisema hatua hiyo kwao ni ushuhuda kuwa mshikamano na bidii vikijumuika, wanaweza kufanya mabadiliko makubwa ya utunzaji na uhifadhi wa mazingira.

Msokolo alitumia nafasi hiyo kuwashukuru wote waliojitokeza kushiriki katika kazi hiyo na kusisitiza kuwa umoja siku zote ni nguvu na kujitoa kwao kuna maana kubwa katika utunzaji wa mazingira chini ya kauli mbiu yao  “‎Tuwe pamoja kulinda fukwe, bahari na mazingira yetu — hatua moja baada ya nyingine”.

Katika kazi hiyo viongozi wa kampuni hizo walishiriki akiwepo Meneja Mkazi wa Kampuni ya Emirates Leisure Retail, Paul Atallah na Meneja Mkazi wa Kampuni ya DNATA,  Maruan Essa ambao kwa pamoja walijumuika na wafanyakazi wao  kufanikisha shughuli hiyo na kuonesha mfano bora wa viongozi wanaojitoa kwenye shughuli za kijamii.

Usafi ukiendelea kufanyika.
Wafanyakazi hao wakiwa na viroba vyenye takataka baada ya kufanya usafi kwenye ufukwe huo.
Usafi ukifanyika.

Kazi ya usafi ikiendelea
Usafi ukifanyika
Afisa Utawala Msaidizi wa Kampuni ya Emirates Leisure Retail Zanzibar, Hussein Ramadhani Layya (Maarufu Msokolo), akiwa amejitwisha kiriba chenye takataka wakati wa ufanyaji huo wa usafi. 

Wafanyakazi wa kampuni hizo hizo wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kufanya kazi hiyo ya usafiWafanyakazi wa kampuni hizo hizo wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kufanya kazi hiyo ya usafi


No comments