Breaking News

WATANZANIA WATAKIWA KUILINDA TUNU YA AMANI.

Mratibu wa mkutano wa Injili utakaofanyika katika Uwanja wa Michezo wa CCM Kirumba Jijini Mwanza Nabii Utukufu, akitoa taarifa ya maandalizi ya Mkutano huo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani)

………………..

Na Hellen Mtereko, Mwanza.

WATANZANIA wametakiwa kulinda amani na utulivu wa nchi kwa kuwa ndio msingi wa maendeleo.

Wito huo umetolewa na Mratibu wa Mkutano wa Injili utakaofanyika nchini Tanzania Nabii Utukufu Kwa bwana Peter, wakati akitoa taarifa ya maandalizi ya Mkutano huo utakaoanza Julai 24, hadi 28 2024 katika uwanja wa michezo wa CCM kirumba uliopo Wilaya ya Ilemela Mkoani Mwanza.

Amesema kuwa amani tuliyonayo ni tunu kubwa sana inayoweza kutupa furaha wakati wote na lengo la Mkutano huo ni kuliombea Taifa la Tanzania ili amani izidi kutawala.

” Taifa hili linamuhitaji Mungu sana na  silaha yoyote inatengenezwa wakati wa amani,hivyo maombi yanayoweza kutusaidia kwenye Taifa letu ni maombi tunayoweza kuyaomba tukiwa kwenye amani na utulivu”, amesema

Amesema Maandalizi ya Mkutano utakaongozwa na Pastor Ezekiel Odero wa Kanisa la New Life Prayer Center kutoka Mombasa Nchini Kenya yanaendelea vizuri kwaajili ya kuhakikisha watu watakauohudhuria wanapata huduma stahiki.

“Matumaini yetu tunaamini watu wengi watafika katika Mkutano huu na mpaka  sasa tumeishanza kupokea simu kutoka kwa mataifa mengine juu ya ujio wao kwenye mkutano huu” Amesema Utukufu

Baadhi ya wananchi wameeleza kuwa wanaamini ujio wa Mkutano huo utawapa uponyaji na kuwafungua kiroho na kupata majibu ya matatizo yao ya muda mrefu.

“Tunaamini ujio wa huyu mchungaji ni faraja kwetu maana tumekuwa tukiangalia kwenye tv na kuona namna watu wanavyoponywa na kufunguliwa kwa maombi na sisi tunaimani hiyo ya kutatuliwa matatizo tuliyonayo hususani ya kiafya”  

No comments