WAZIRI UMMY AWASILISHA UJUMBE WA RAIS SAMIA KWA RAIS WA GUINEA
Na WAF - Guinea
Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu (Mb) ambae pia ni Mjumbe Maalum wa Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amewasilisha ujumbe kwa Rais wa Jamhuri ya
Guinea Mhe. General Mamadi Doumbouya uliotoka kwa Rais wa Tanzania Dkt. Samia
Suluhu Hassan.
Waziri @ummymwalimu amewasilisha ujumbe wa Rais Samia Julai 10, 2024 ambao
umepokelewa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Guinea Mheshimiwa Dkt.
Morrisanda Kouyate.
Wakati akikabidhi ujumbe huo Waziri Ummy amesema ili kudhihirisha urafiki
wa kidugu kati ya Guinea na Tanzania kuna barabara kubwa katika Jiji la Dar es
salaam inayoitwa Toure Road na Hospitali ya Sekou Toure iliyopo Jijini Mwanza
ambao ni mji wa pili kwa ukubwa nchini Tanzania wakati nchini Guinea kuna Chuo
Kikuu cha Julius Nyerere University of Kankan (UJNK).
"Naishukuru sana Serikali ya Jamhuri ya Guinea kwa mapokezi mazuri
ambayo yamedhihirisha ushirikiano wetu wa karibu na hatimaye kupokea ujumbe
Maalum wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu
Hassan." Ametoa shukrani hizo Waziri Ummy
Wakati akipokea ujumbe huo kutoka Nchini Tanzania kwa niaba ya Rais wa
Guinea, Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Guinea Mheshimiwa Dkt. Morrisanda
Kouyate amesisistiza kuwa, Jamhuri ya Guinea itaendelea kutambua ushirikano wa
kidugu na wa muda mrefu kati ya Guinea na Tanzania ulioanzishwa wakati wa
waasisi ya Mataifa hayo Mawili, Hayati Baba wa Taifa Mwl. Julius Nyerere na
Mhe. Ahmed Sekou Toure.
No comments