Breaking News

DKT. ZAKIA ABUBAKAR: WAANDIKISHAJI WAPIGA KURA TOENI KIPAUMBELE KWA MAKUNDI MAALUMU

Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Dkt. Zakia Abubakar akifunga mafunzo ya Maafisa Uandikishaji Ngazi ya Jimbo, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ugavi na Maafisa Teknolojia ya Habari (TEHAMA) wa Halmashauri Mkoa wa Singida yaliohusu Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura yaliyoanza Septemba 14, 2024 na kufikia tamati Septemba 15, 2024 katika Ukumbi wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) Kampasi ya Singida.

.....................................

Imeandaliwa na Dotto Mwaibale

(0754-362990)


MJUMBE wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Dkt. Zakia Abubakar amewataka Maafisa Uandikishaji Ngazi ya Jimbo, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ugavi na Maafisa Teknolojia ya Habari (TEHAMA) wa Halmashauri Mkoa wa Singida kuyapa kipaumbele makundi maalumu kama vile wazee, walemavu, wajawazito na watoto wadogo wakati wa zoezi la kuwaandikisha wapiga kura.

Dkt. Abubakar ambaye alikuwa mgeni rasmi ameyasema hayo wakati akifunga mafunzo kwa watendaji hao ngazi ya mkoa yaliyohusu uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura yaliyoanza Septemba 14, 2024 na kufikia tamati Septemba 15, 2024 katika Ukumbi wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) Kampasi ya Singida.

Pia amewataka maafisa hao kuwepo vituoni muda wote hata kama hakutakuwa na waombaji ambao watajitokeza kuomba kujiandisha.

Dkt. Abubakar aliwaambia maafisa hao kuwa mafunzo hayo waliyoyapata yatawasaidia kutekeleza majukumu yao kwa nadharia na vitendo  kwa yale yote waliyofundishwa na kuwa  wanapaswa kutekeleza majukumu waliyopewa kwa kuzingatia Katiba ya Nchi, Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani na kanuni zilizotungwa chini ya vipengere vya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.

“Napenda kutoa wito kwenu nyote kuendelea kutoa muda wenu wa ziada kusoma na kupitia maelekezo yote mliyopewa ili kuongeza uelewa kuhusu wajibu na majukumu yenu ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura,” alisema Abubakar.

Aidha, Dkt. Abubakar aliwaambia maafisa hao kuwa wakumbuke kwamba maelekezo yote waliyopewa ni zana za kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kuwa wanahimizwa kuwahamasisha wananchi wenye sifa ili wajitokeze kujiandisha na kupata haki yao ya kikatiba itakayowawezesha kuwachagua viongozi wao.

.Alisema matarajio ya Tume ni kuwa mara baada ya zoezi hilo kukamilika watu watakao kuwa wamepatiwa kadi watakuwa ni wapiga kura halali.

“Jukumu la uhamasishaji linawahusu moja kwa moja ninyi watendaji kwa kushirikiana na wadau wengine katika maeneo yenu na kupitia nyenzo mlizonazo nasisitiza mabango na vipeperushi mtakavyopewa na Tume mvisambaze mapema katika kata zote zilizopo kwenye halmashauri zenu na kazi yenu kubwa ni kusimamia na kuendesha shughuli zote za uboreshaji kwenye maeneo yenu,” alisema Dkt. Abubakar.

Dkt. Abubakar aliwataka maafisa hao kusoma kwa makini Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, sheria za uchaguzi, kanuni za uboreshaji, maelekezo na miongozo yote inayotolewa na Tume ili kazi yao ifanyike kwa udhanifu na haki na wasisite kuwasiliana na Tume kwa ajili ya ufafanuzi wa masuala yoyote yanayohusiana na utekelezaji wa majukumu yao.

Alisema Tume Huru ya Uchaguzi (INEC) imetekeleza majukumu yake katika hatua ya mafunzo na wao wanawajibu wa kuhakikisha wanayatekeleza yote kwa maendeleo ya nchi.

Dkt. Abubakar alitoa wito kwa maafisa hao kufuatilia kwa karibu zoezi hilo na kushiriki kikamilifu na kuhakikisha linafanikiwa na kuwa makini katika eneo la usambazaji na utunzaji wa vifaa na muda sahihi wa ufunguaji na ufungaji wa vituo vya kuwaandikishia wapiga kura na vilevile kuwasisitiza watendaji waliochini yao kutumia lugha nzuri.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa mafunzo hayo ambaye pia ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, Michael Matomora alisema sasa wapo tayari kwenda kuyafanya kwa ujuzi na weledi mkubwa yale yote waliyojifunza.

“ Tunaihadi Tume tunaenda kushiriki zoezi hili kwa uadilifu wa hali ya juu tukifahamu kwamba tumetakwa kulifanya pasi kutoa siri, sisi sasa ni sehemu ya Tume na tutakuwa makini kwa kutunza siri hadi hapo Tume itakapoona inafaa kutoa taarifa hiyo,” alisema Matomora.Mwenyekiti wa mafunzo hayo ambaye pia ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, Michael Matomora, akitoa neno la shukurani baada ya kumalizika kwa mafunzo hayo


Mafunzo yakiendelea.
Washiriki wakiwa kwenye mafunzo hayo. Kutoka kushoto ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Singida, Ester Chaula na  kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Singida, Joanfaith Kataraia.
Mafunzo yakiendelea.
Washiriki wakiwa kwenye mafunzo hayo.
Mafunzo yakiendelea.
Taswira ya mafunzo hayo.
 

No comments