Breaking News

ORYX GAS, TULIA AKSON WAKABIDHI MITUNGI 1000 KWA MAMA NA BABA LISHE MBEYA

SERIKALI imetenga fedha kwaajili ya kuendelea kugawa nishati mbadala ya kupikia kwa wananchi ili kuondokana na matumizi ya kuni na mkaa ambayo yamekuwa na athari za kiafya na kimanzingira kwa watumiaji.


Ameyasema hayo leo Agosti 31,2024 Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga wakati akihitimisha mashindano ya kupika kwa gesi ya Oryx Mama na Baba Lishe 1000 mkoani Mbeya ambapo washiriki pia walikabidhiwa mitungi na majiko yake ya kupikia.


Naibu Waziri Judith Kapinga aliyekuwa mgeni rasmi amesema Serikali imekuwa na mikakati mbalimbali ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini na lengo ifikapo mwaka 2034 asilimia 80 ya wananchi wawe wanatumia nishati mbadala katika kupikia.


" Moja ya maombi ya wananchi kwa wadau wa gesi ni kupunguzwa kwa bei ya gesi ambayo kwa sasa ni kubwa.Tunashauri wadau katika sekta hii ya gesi tengenezeni mfumo ambao utawezesha Mwananchi kununua gesi kidogo kidogo kwa siku badala ya kutoa fedha nyingi kwa wakati mmoja,"amesema.


Amesisitiza kukiwa na uwezo wa gesi kununuliwa kidogo kidogo anaamini wananchi wengi watatumia gesi na hivyo kusaidia kupunguza Kasi ya uharibu wa mazingira lakini pia kulinda afya za wananchi.


Kuhusu tamasha hilo la mapishi , Naibu Waziri Kapinga amempongeza Dk.Tulia Ackson kuandaa mashindano hayo makubwa na kushirikisha Mama na Baba Lishe 1000 kushindana kupika kwa gesi kwani yamekuwa ya mfano na yametumika kutoa elimu ya nishati na utunzaji mazingira.


Pia amesema kumekuwa na dhana kupika kwa kuni na mkaa ndio chakula kinakuwa kitamu lakini ukweli chakula kinachopikwa kwa nishati mbadala kama gesi ni kitamu na kinaladha.


Ametumia nafasi hiyo kuwashukuru Oryx kwa kuendelea kuishika mkono Serikali katika kusaidia kuhamasisha nishati safi ya kupikia,wanafanya kazi nzuri na wamekuwa wakifika kila mahali wakigawa mitungi na majiko yake kwa jamii.


Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Oryx Gas Tanzania Benoit Araman amesema lengo kuu la mashindano ya mapishi ni kuhamasika matumizi ya nishati safi kwa lengo la kulinda mazingira ambayo yamekuwa yakiharibiwa kwasababu ya kukata kuni na mkaa.


"Kwa miaka zaidi ya 15 iliyopita upatikanaji wa nishati ya kupikia umekuwa ukipangwa na kujadiliwa lakini hivi sasa Serikali inayoongozwa na Rais DK.Samia Suluhu Hassan amekuwa na hamasa kubwa ya kuhimiza wananchi kutumia nishati safi ya kupikia.


"Oryx Gasi tunaamini kupika kwa gesi kunakwenda kusaidia kulinda mazingira sambamba na kupunguza muda mwingi kwa wanawake kuwa porini kutafuta kuni na mkaa kwa ajili ya kuanda chakula.Pia kupika kwa gesi kutasaidia kuwalinda wanawake dhidi ya wanyama wakali walioko misitu lakini kuwalinda dhidi ya vitendo vya ukatilii ambavyo wanakutana navyo wakiwa porini."Amesema Benoit.


Ameongeza pamoja na kusaidia makundi mbalimbali kuyawawezesha kupata mitungi ya gesi ya Oryx lakini wanajivunia kuwafikia Mama na Baba Lishe zaidi ya 12000 ambao wamepata elimu ya matumizi salama ya kupika kwa gesi sambamba na kuwapatia mitungi midogo na mikubwa kwa lengo la kuwawezesha kufanya shughuli za mapishi kwa urahisi na kuwa salama kiafya,"amesema.


Pamoja nayo hayo amesema kubalika kutoka kutumia kuni na mkaa hadi kupika kwa gesi kunatafsiri kubwa ya kwamba nchi imepiga hatua kubwa ya kimaendeleo na kusisitiza oryx Gas itaendelea kuhamasisha nishati safi ili kufikia malengo ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ifikapo mwaka 2034 asilimia 80 ya wananchi wawe wanatumia nishati safi.


Awali akizungumza kwa niaba ya Machifu Mkoa wa Mbeya, Chief Chief Rocket Mwashinga amewaomba viongozi wa Serikali na wadau wa gesi kuangalia uwezekano wa kupunguza bei ya gesi ili wananchi waweze kumudu gharama kwani kwa sasa bado iko juu.


"Gesi ipunguzwe bei ili wananchi tuokoe mazingira kwani bei ikiwa kubwa wataendelea kushambulia misitu na kuharibu mazingira.Mazingira ni muhimu sana na sisi Machifu tuko maeneo ya pembezoni mwa Mkoa ambako kuna miti niwahakikishie machifu na viongozi wote wa kimila nchini tunaouwezo mkubwa wa kulinda mazingira,kikubwa tunaomba tuwezeshwe."


Kwa upande wao baadhi ya Mama na Baba Lishe walioshiriki mashindano ya kupika kwa gesi wamesema kupitia mashindano hayo wamenufaika na mafunzo waliyoyapata sambamba na kuelezwa umuhimu wa kutunza mazingira na wanatoa shukrani kwa waandaaji wakiongozwa na Spika wa Bunge na Mbunge wa Jimbo la Mbeya Mjini Dk.Tulia Ackson.

No comments