WAZIRI MKUU: SUALA LA MAZINGIRA LIWE AJENDA YA KITAIFA
“Na tunapokwenda kuhifadhi mazingira lazima tuanze na ngazi ya familia na
tunapopanda juu tupanue wigo hadi kwa wadau mbalimbali. Viongozi wa dini mnayo
nafasi kubwa na hii lazima iwe ajenda maalum, iwe ni ofisi za umma, za binafsi
au kwenye taasisi.”
Ametoa kauli hiyo leo (Jumanne, Septemba 10, 2024) wakati akifunga mkutano
maalum wa viongozi na wadau wa mazingira ulioitishwa ili kujadili mwenendo wa
mazingira nchini. Mkutano huo ulifanyika kwenye Kituo cha Mikutano cha Jakaya
Kikwete, jijini Dodoma.
Amesema kitendo hicho kitakuwa ni kuunga mkono juhudi za Rais Dkt. Samia
Suluhu Hassan za kuendelea kuimarisha uhifadhi na Usimamizi wa mazingira
nchini, kazi aliyoifanya kwa weledi, ustadi na mafanikio tangu akiwa Makamu wa
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
“Amemudu kusimamia na kutoa miongozo mahsusi ya kuhakikisha mazingira
yanahifadhiwa. Leo hii, yeye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
tunamuona anaendelea kulisimamia ili Taifa lifanikiwe katika uhifadhi wa
mazingira kwa vizazi vya sasa na baadaye,” amesema.
Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwaeleza wajumbe wa mkutano huo juu ya
jitihada ambazo Rais Dkt. Samia amekuwa akizichukua ili kuhakikisha suala la
nishati safi linakubalika.
"Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amekuja na dhana mpya ya
kukataa kukata miti na kutuhamasisha kuhusu nishati safi ya kupikia. Rais wetu
amekuwa kinara wa nishati safi hadi na mwezi Mei alienda Ufaransa kuhutubia
kuhusu nishati safi na yeye akiwa ni Mwenyekiti mwenza wa mkutano huo. Hii ni
fahari kwa nchi yetu," amesema.
Amesema Serikali imetoa fursa kwa wajasiriamali kuanzisha biashara ya kuuza
mitungi na majiko ya gesi hadi kwenye ngazi ya vijiji ili nishati hiyo iweze
kupatikana kwa urahisi. “Huko mbele tutaweka ukomo wa matumizi ya mkaa na
kuni,” ameongeza
No comments