Breaking News

RAIS MWINYI: SMZ IMEWEKEZA KATIKA MIUNDOMBINU YA AFYA

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi, akizungumza na Meneja Mwandamizi wa Mfuko wa Dunia (Global Fund), Dk. Sara Asiimwe, na ujumbe wake ulioongozwa na Waziri wa Afya, Nassor Ahmed Mazrui.

.............................

Na Mwandishi Wetu, Zanzibar


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema kuwa Serikali imewekeza kwa kiwango kikubwa katika miundombinu ya afya kutokana na umuhimu wa sekta hiyo kwa jamii.

Rais Dk. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 15 Oktoba 2024, Ikulu, Zanzibar, alipokutana na Meneja Mwandamizi wa Mfuko wa Dunia (Global Fund), Dk. Sara Asiimwe, na ujumbe wake ulioongozwa na Waziri wa Afya wa Zanzibar , Nassor Ahmed Mazrui.

Aidha, Rais Dk. Mwinyi ameishukuru “Global Fund” kwa jitihada zake za kuiunga mkono Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuisaidia kwenye masuala mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo sekta ya afya.

Halikadhalika, Rais Dk. Mwinyi amepongeza juhudi za “Global Fund” za kuisaidia Zanzibar katika sekta ya afya na nyingine za maendeleo, akisisitiza kuwa zinasaidia jitihada za Serikali anayoiongoza katika kutekeleza azma ya kutoa huduma bora za afya.

Akizungumzia huduma ya bima ya afya kwa wageni wanaoingia Zanzibar, Rais Dk. Mwinyi ameeleza kuwa Serikali ina dhamira ya kuanzisha bima hiyo kutokana na umuhimu wake kwa wageni, hivyo ameomba Mfuko huo uangalie namna ya kuiunga mkono Serikali.

Naye, Dk. Sara Asiimwe alimueleza Rais Dk. Mwinyi kuwa “Global Fund” inafanya kazi kwa karibu na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia sekta zake za maendeleo, ikiwemo Wizara ya Afya. Aidha, aliahidi kuwa taasisi yao itaendeleza ushirikiano na Zanzibar, hasa katika miradi ya maendeleo.

Mazungumzo yakiendelea
Meneja Mwandamizi wa Mfuko wa Dunia (Global Fund), Dk. Sara Asiimwe, akizungumza.

Kikao kikiendelea.

Waziri wa Afya wa Zanzibar , Nassor Ahmed Mazrui. akizungumza kwenye kikao hicho.


 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi na Meneja Mwandamizi wa Mfuko wa Dunia (Global Fund), Dk. Sara Asiimwe (katikati) , na ujumbe wake ulioongozwa na Waziri wa Afya, Nassor Ahmed Mazrui (wa pili kulia), wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kufanyika kwa kikao Ikulu Zanzibar.

No comments