Breaking News

DC KILOSA: JESHI LA AKIBA NI NGUZO MUHIMU YA USALAMA NCHINI

Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Shaka Hamdu Shaka, akikagua gwaride  wakati  akifunga mafunzo miezi nne ya askari 114  mkupuo wa 20 wa Jeshi la Akiba yaliyofanyika katika Viwanja vya Shule ya  Msingi Mvumi wilayani humo Agosti 15, 2025.

.........................................

Na Dotto Mwaibale

MKUU wa Wilaya ya Kilosa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Shaka Hamdu Shaka amesema Jeshi la Akiba ni nguzo muhimu katika kujenga mfumo wa usalama ndani ya Taifa letu.

Shaka ameyasema hayo Agosti 15, 2025 wakati  akifunga mafunzo ya miezi 4 ya askari 114  mkupuo wa 20 wa Jeshi la Akiba yaliyofanyika katika Viwanja vya Shule ya  Msingi Mvumi wilayani humo.

Alisema jeshi hilo kama alivyosema Luteni Kanali Ramadhani ni sehemu ya akiba yetu muhimu pale ambapo itatokea dharura kwa kwenda kuunganisha nguvu katika Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

“Nichukue nafasi hii kulishukuru Jeshi la Kujenga Taifa Makao Makuu kwa kuratibu mafunzo haya na kuendelea kuwaandaa askari  ili kuwa na akiba ya kutosha katika nchi yetu na kujihakikishia usalama wetu hata pale litakapotokea tishio watanzania na mipaka ya nchi yetu itabaki kuwa salama,” alisema Shaka.

Aliwataka wahitimu wa mafunzo hayo kwenda kuzingatia maadili na kuwa waaminifu kwa jamii kama walivyofundishwa na kuwa watatuzi wa changamoto zao na kuifanya jamii kuendelea kuwa na umoja, upendo na mshikamano.

Shaka alisema Serikali haitasita kuchukua hatua za kinidhamu kwa muhitimu yeyote wa mafunzo hayo atakayeenda kufanya kinyume na kiapo alichokiapa wakati wa kutumikia taifa na kueleza kuwa kiapo hicho kikawe shuhuda kwao na kwa Mwenyezi Mungu.

Shaka alisema usalama wa nchi ni nguzo ya maendeleo na kuwa wahitimu hao wanatakiwa kwenda kuimarisha nguzo hiyo kwa ajili ya mustakabaIi wa taifa letu.

Alisema Wilaya ya Kilosa haipo kisiwani na kuwa inachangamoto kadhaa kama za wananchi kujichukulia sheria mkononi, wizi wa kuvunja, migogoro ya ardhi na nyingine nyingi hivyo ni wajibu wao kwenda kusaidiana na vyombo vingine vya usalama na kuhakikisha wilaya hiyo inabaki kuwa salama.

Aliwataka askari hao wa jeshi la akiba kwenda kushirikiana na vyombo vingine vya usalama wakati wa uchaguzi mkuu utakaofanyika mwishoni mwa mwaka huu na kuhakikisha unafanyika kwa amani na utulivu. 

Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Shaka Hamdu Shaka, akihutubia wakati akifunga mafunzo hayo. 
Wananchi wakishiriki hafla ya kufunga mafunzo hayo.
Askari wa Akiba wakiwa  katika ufungaji wa mafunzo hayo.
Gwaride maalumu la askari wa akiba likipita mbele ya mgeni rasmi. 

No comments