Breaking News

UKOSEFU WA UWAJIBIKAJI CHANZO CHA RUSHWA YA NGONO VYUONI

Afisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Mkoa wa Singida, Benjamini Masyaga akizungumza na wanafunzi wa mwaka wa kwanza wa msimu wa masomo 2025/ 2026 wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) Kampasi ya Singida Novemba 19, 2025.

...........................

Na Dotto Mwaibale, Singida

UKOSEFU wa Uwajibikaji na Uwazi katika Mifumo ya Chuo imeelezwa kuwa ni sababu za kuwapo kwa rushwa ya ngono Vyuoni.

Hayo yameelezwa na Afisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Mkoa wa Singida, Benjamini Masyaga wakati akizungumza na wanafunzi wa mwaka wa kwanza wa msimu wa masomo 2025/ 2026 ‘Orientation for first year students’ katika Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) Kampasi ya Singida Novemba 19, 2025.

“ Pale ambapo hakuna ufuatiliaji wa walimu, taratibu za alama hazipo wazi, au mawasiliano kati ya wanafunzi na uongozi ni dhaifu, rushwa ya ngono hujitokeza kwa wingi,” alisema Masyaga.

Alisema Vyuo vinaposhindwa kuwaadhibu hadharani wahusika, mazingira yanayotia moyo rushwa ya ngono huendelea.

Masyaga alitaja sababu nyingine inayofanya vitendo vya rushwa ya ngono iendelee ni baadhi ya wahalifu kurudi vyuoni baada ya kuhamishwa bila adhabu.

Alitaja sababu nyingine ni ile ya ushawishi kwani baadhi ya wanafunzi hasa wanaoingia chuo kwa mara ya kwanza, huathiriwa na marafiki wanaoona ngono kama njia ya kupata msaada, hivyo kupunguza uwezo wa kutambua ukatili au rushwa.

Masyaga alisema ili kuzuia na kupambana na rushwa ya ngono inatakiwa Elimu na Uhamasishaji kwa wanafunzi itolewe kupitia warsha za mara kwa mara.

Alieleza jambo lingine ni kuwepo kwa uadilifu wa kitaaluma, haki na wajibu wa mwanafunzi na namna ya kuiripoti rushwa ya ngono pamoja na kuanzisha kozi fupi za Ethics and Anti- Corruption kw wanafunzi wapya (Orientation)

Afisa huyo wa Takukuru alitaja baadhi ya njia nyingine za kupambana na rushwa ya ngono ni kuimarisha mfumo wa uongozi na usimamizi wa chuo kwa kuanzisha taratibu za wazi na shirikishi katika utoaji wa alama, usajili, malazi, udahili, mitihani na huduma nyingine.

Alisema matumizi ya mfumo wa kidijitali (online systems) unasaidia kupunguza mwingiliano wa ana kwa ana unaowez kuchochea rushwa.

Alitaja njia nyingine kuwa ni kuanzishwa na kuimarisha Dawati la Malalamiko kwa chuo husika kuwa na dawati huru ambalo litapokea taarifa bila ya kuvuja na wanafunzi wapewe njia salama za kuripoti na kuweka kanuni za kulinda mtoa taarifa.

Aidha, Masyaga alisema Serikali ya Wanafunzi iwe na mafunzo ya maadili, uwajibikaji na uongozi bora na kuweka mifumo ya uwazi katika matumizi ya fedha za wanafunzi na miradi ya serikali hiyo. Wanafunzi wa mwaka wa kwanza TIA Singida wakisikiliza mada iliyohusu rushwa ya ngono vyuoni iliyokuwa ikitolewa na Afisa wa Takukuru, Benjamini Masyaga, 

No comments