Breaking News

WANAFUNZI: TAASISI YA UHASIBU SINGIDA MAHALI PAZURI KUPATA ELIMU

Mwanafunzi wa mwaka wa kwanza ngazi ya cheti,  Emmanuel Marko akizungumza.

.......................................

Na Dotto Mwaibale, Singida

TAASISI ya Uhasibu Tanzania (TIA), Kampasi ya Singida imetajwa kuwa ni mahali pazuri kupata elimu kutokana na kozi mbalimbali zinazotolewa na maboresho mazuri ya miundombinu.

Hayo yamebainishwa na Emmanuel Marko Mwanafunzi wa mwaka wa kwanza ngazi ya cheti wa Taasisi hiyo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari wakati wa ‘Orientasion for First Year Students’ iliyofanyika Novemba 20, 2025.

“Niwaombe wazazi na walezi wawalete watoto wao kuja kupata mafunzo ya kozi mbalimbali kwenye chuo hiki kwani ni mahali sahihi pa kupata elimu itakayo wasaidia katika maisha yao,” alisema Marko.

Aidha, Marko alisema chuo hicho kina mazingira mazuri ya kujifunzia walimu na wafanyakazi wake chini ya Mkurugenzi wa Kampasi hii Dkt. James Mrema ni wakarimu wamewapokea vizuri hivyo wanatoa shukurani zao kwao.

Marko alisema tangu walipofika baada ya chuo hicho kufunguliwa kwa ajili ya msimu wa masomo wa mwaka 2025/ 2026 wameelekezwa mambo kadha wa kadha kama kuwa na nidhamu na kutojihusisha na vitendo mbalimbali ambavyo haviendani na maadili.

Alivitaja baadhi ya vitendo hivyo kuvaa mavazi yasiyo na staha ya kubana miili yao wakati wakiwa chuoni na maeneo mengine nje ya chuo, kuvaa fulana, kofia aina kapero, kaptura au suruali chini ya makalio ‘Kata K’ na kunyoa kiduku.

Aliyaeleza mambo mengine walioelekezwa ni kutojihusisha na vitendo vya mahusiano ya kimapenzi, uvutaji wa bangi, kutoka chuoni bila ya ruhusa na kusisitiziwa kuzingatia masomo wakati wote kwani ndilo jambo ambalo limewapeleka chuoni hapo na si vinginevyo.

Marko alitumia nafasi hiyo kuipongeza Serikali kupitia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kufanya uwekezaji mkubwa katika chuo hicho ambacho kinatoa fursa ya kupata elimu kwa watoto na makundi mengine ya watanzania.

Kwa upande wake Rais wa Serikali ya Wanafunzi (TAISO), Maiba Loitare amewasisitizia wanafunzi hao kuzingatia masomo na kufuata taratibu na sheria za chuo.

Aidha, aliupongeza uongozi wa kampasi hiyo kwa kuweka utaratibu wa kutoa matangazo Stendi Kuu ya Mabasi ya Mkoa wa Singida Misuna kwa ajili ya kuwaelekeza wanafunzi wageni namna ya kufika katika chuo hicho bila ya kupata usumbufu.

Loitare aliipongeza Serikali kwa kuboresha miundombinu ya chuo hicho na kukifanya kuwa sehemu ya mvuto kupata masomo kwani imeipatia taasisi hiyo Sh. Bilioni 13. 5 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la taaluma ambao ujenzi wake unaendelea kwa kasi chini ya Mkurugenzi wa TIA Singida Dkt. James Mrema.

Afisa Utumishi na Msimamizi wa Huduma za Rasilimali Watu na Utawala wa Taasisi hiyo, Sanura Mohamed akizungumza na wanafunzi hao aliwaambia   taratibu zote za namna ya kufanya wakiwa chuoni hapo zimeweka bayana ili kila mwanachuo azielewe hivyo ni wajibu wao kuzifuata.

Sanura alisema TIA Singida ni moja ya kampasi ambayo inapokea wanafunzi kutoka kila mkoa na kueleza kuwa udahili wa wanafunzi umekuwa ukiongezeka kila mwaka.

Alitaja kozi zinazotolewa na chuo hicho kuwa ni Accountancy , Procurement and logistic management, Human resource management, Business Administration na Marketing and public relation.

Aidha, Sanula alisema kozi zote hizo zinaanzia ngazi ya cheti mpaka masters.

Kwa mawasiliano zaidi kuhusu chuo hicho unaweza kupiga simu namba 0752540341 au kupitia mtandao wao (Website) www.tia.ac.tzRais wa Serikali ya Wanafunzi (TAISO) wa chuo hicho, Maiba Loitare,akizungumza.

Afisa Utumishi na Msimamizi wa Huduma za Rasilimali Watu na Utawala wa Taasisi hiyo, Sanura Mohamed, akizungumza.
Mwanasheria wa TIA Singida Wakili Joseph Wawa akizungumza na wanafunzi hao.
Wanafunzi wa mwaka wa kwanza wakiwa kwenye tukio hilo. 

No comments