Breaking News

DKT. NOELIA ANSGARY MYONGA AANDIKWA KWENYE RAMANI YA AMANI DUNIANI

Mgeni Rasmi Balozi Prof. Askofu Rejoice Ndalima akimkabidhi cheti  Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Balozi Dr Noelia Myonga ambaye ni Mkuu wa Ofisi ya Mahusiano TANAPA Dodoma cha kutambua mchango wake katika Taifa wa kuhifadhi mazingira.

...........................

Na Doto Mwaibale 

KATIKA jukwaa lililojaa heshima, ishara za matumaini, na alama za mabadiliko, mwanamke mmoja amepanda kilele cha mafanikio sio kwa kupigiwa makofi tu, bali kwa kutia sahihi historia mpya ya Tanzania na dunia.

Katika ukumbi wa Rungwe Hotel, Dar es Salaam, mbele ya macho ya watu wenye nafasi, wawakilishi wa taasisi, wanaharakati wa amani na viongozi wa kimataifa Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Balozi Dkt. Noelia Ansgary Myonga kwa sasa ni Mkuu wa Ofisi ya Mahusiano Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) Myonga, amepewa rasmi heshima anayostahili kwa kutunukiwa hadhi ya  Balozi wa Amani Duniani (AMB) "Peace Ambassador (AMB)" na Greenling Peace Foundation.

Sio tu kwa sababu alifanikiwa, bali kwa sababu amefanikiwa 'kwa kiwango cha dunia'. Dkt. Noelia si jina jipya katika majukwaa ya uongozi, ulinzi wa maliasili, utalii, mazingira na ustawi wa jamii.

Lakini safari yake kuelekea nafasi ya Balozi wa Amani Duniani (AMB) ni hadithi ya ujasiri, moyo wa utumishi, hekima na uthubutu wa mwanamke ambaye hakupambana tu kwa ajili ya mafanikio yake, bali kwa ajili ya mustakabali wa sekta ya uhifadhi, Taifa, Bara la Afrika na dunia nzima.

 Leo, jina lake limeunganishwa na alama ya heshima ya kimataifa, kama mwanamke wa kwanza na mtumishi wa kwanza kutoka sekta ya Uhifadhi nchini Tanzania kutwaa taji hili kubwa duniani.

Katika hotuba ya tuzo hiyo, ilisisitizwa kuwa mchango wake umejikita si tu katika kulinda mazingira, bali kuunganisha Uhifadhi na Amani—dhana mbili ambazo kwa kawaida hazipewi nafasi ya kutazamwa pamoja, lakini kwake zimekuwa mihimili ya maisha na utumishi.

Alitambuliwa kwa mchango wake wa kipekee kwenye diplomasia ya mazingira, kujenga mahusiano ya kijamii, kuchochea maridhiano kati ya jamii na uhifadhi, na kukuza ufahamu kuwa amani huanzia kwenye kuheshimu uhai—ikiwemo ardhi, wanyama, misitu, mito, na mwanadamu.

Tunapomwangalia Dkt. Noelia, hatumuoni kama tu kiongozi wa serikali, bali tunaona alama ya kizazi kipya cha uongozi chenye ubunifu, maadili, na roho ya ibada katika utumishi wa jamii.

Anaamini amani si hotuba; ni matendo. Si nadharia; ni utendaji. Si tathmini; ni uwajibikaji. Na leo hii, dunia imesimama kumshuhudia akiwa na hadhi mpya, si tu kama Kamishna, Dkt., au Mtaalamu wa Uhifadhi—bali sasa AMBASSADOR OF GLOBAL PEACE.

Zaidi ya heshima binafsi, tuzo hii ni ushahidi kwamba sekta ya Uhifadhi ina mchango mkubwa zaidi ya kuona wanyama pori na hifadhi za Taifa.

Kupitia yeye, Tanzania sasa imefungua dirisha jipya la diplomasia ya kimataifa—ambapo Uhifadhi unakuwa nguzo ya kujenga amani duniani, kukuza utalii wa kidiplomasia, na kuitangaza nchi kimataifa kwa sababu ya majibu ya changamoto za mazingira kwa njia zenye kuleta maridhiano, matumaini na ushirikiano wa kimataifa.

Dkt. Noelia ni kielelezo cha namna mwanamke anaweza kuhimili dhamana kubwa katika dunia inayodai uthibitisho wa ubora.

Ni mfano wa kuigwa kwa wasichana wanaoota kuwa viongozi wa kimataifa, kwa wanawake wanaotamani kuvuka mipaka ya kimaamuzi, na kwa watumishi wanaoamini thamani ya utumishi ni faraja ya jamii na si tu nafasi ya vyeo.

Ameandika historia—safari isiyopimika kwa cheo, bali athari. Leo, tunasema kwa sauti ya matumaini, sauti ya shukrani, na sauti ya heshima: Huyu ni mwanamke ambaye ameiambia dunia kuwa Tanzania ina sauti ya amani.

Sekta ya uhifadhi ina balozi. Na mwanamke anaweza—anaweza kuongoza, kuleta amani, na kubeba bendera ya Taifa katika majukwaa makubwa duniani.

Dkt. Noelia ni  Mtumishi na Mwanamke wa kwanza kuwa Balozi kwenye Sekta za Uhifadhi hivyo nafasi hiyo itaendeleza kuitambulisha vema Sekta ya Uhifadhi na Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania Kimataifa. 

Mafanikio yote hayo yanatokana na uongozi dhabiti wa Kamishna wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA ), Alhaj Musa N.K Juma na kuwezesha kuleta Tuzo nyingine ya kipekee ya kimataifa na hivyo kudhibitisha 'TANAPA NI NYUMBANI.PA TUZO'

Kwa mafanikio hayo Kamishna Juma anapongezwa pamoja na Menejimenti yote ya TANAPA  kwa kuunga mkono jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa akihimiza kutunza rasilimali za nchi zikiwemo Hifadhi kwa maendeleo ya uchumi wa Taifa.

mMwenyekiti Mwanzilishi wa Greeling Global Peace Organization Zambia Prof Bishop Kennedy Songwe akimvika beji Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) Balozi Dr Noelia Myonga ambaye ni Mkuu wa Ofisi ya Mahusiano TANAPA Dodoma.

Mwenyekiti Mwanzilishi wa Greeling Global Peace Organization Zambia Prof Bishop Kennedy Songwe, akimpongeza  Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi  wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Balozi Dr Noelia Myonga ambaye ni Mkuu wa Ofisi ya Mahusiano TANAPA Dodoma  kwa kupata tuzo hiyo.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Balozi Dr Noelia Myonga ambaye ni Mkuu wa Ofisi ya Mahusiano TANAPA Dodoma  akiwa kwenye hafla ya kutunukiwa tuzo.

 

No comments